Home » » Serikali yakubali kuwakutanisha wadau wa sukari

Serikali yakubali kuwakutanisha wadau wa sukari

SERIKALI imesalimu amri baada ya tishio la wazalishaji wa sukari nchini kufunga viwanda vyao iwapo hatua madhubuti za kukabiliana na uingizwaji holela wa sukari kutoka nje ya nchi bila kulipiwa ushuru, hazitachukuliwa.
Baada ya tishio hilo serikali sasa imekusudia kuitisha mkutano wa wazalishaji, wawekezaji, wafanyabiashara wanaoingiza sukari hiyo na walaji ili kujadili changamoto ya kufurika kwa sukari ya nje katika soko la ndani.
Waziri wa Kilimo, Chakula na Ushirika, Christopher Chiza, alisema kutokana na changamoto hiyo wizara yake inakusudia kuandaa mkutano wa kitaifa ili kutafuta namna sahihi ya kulikabili jambo hilo.
Chiza alisema lengo la mkutano huo ni kujenga mazingira rafiki na kuridhisha kila upande kwani lengo ni kuhakikisha viwanda vya ndani vikiendeleza uzalishaji wake huku vikitoa ajira kwa Watanzania.
Kwa upande wake Ofisa Mtendaji na Utawala wa Kiwanda cha Sukari Moshi (TPC) Jafary Ali alisema kiwanda chake kimelazimika kuomba maghala binafsi kwenye mikoa ya Arusha na Kilimanjaro ili kuhifadhi sukari yao.
Alisema uwezo wa kiwanda ni kuhifadhi tani 13,000 kwa wakati mmoja lakini hadi sasa wamezalisha tani 20,000 na kulazimika kuomba kuhifadhiwa tani 7,000 baada ya kukosa soko la ndani.
Ofisa huyo alisema sukari inayozalishwa nchini inauzwa kwa wastani wa sh 69,000 hadi sh 75,000 kwa mfuko wa kilogramu 50 wakati sukari inayotoka nje inauzwa kwa sh 50,000 kwa mfuko wenye ukubwa hiyo jambo linalosababisha sukari ya ndani kukosa soko.
Kwa mujibu wa Ally hivi sasa ipo sukari inayoingia kwa wingi katika soko ijulikanayo kama ‘sukari isiyolipiwa kodiambayo haina vibali vya bodi ya sukari na kutaka serikali inapaswa kujua inaingiaje.
“Kuna sukari nyingine inakuja kwa ajili ya matumizi ya viwanda ambavyo havitumii ‘brown sugarsasa hii ‘industrial sugarinakuja kwa ujanja; ujanja unatumika badala ya kuleta sukari nyeupe kwa ajili ya matumizi ya viwanda wanaleta sukari kama ile tunayozalisha nchini,” alisema.
Alitaja aina ya sukari inayoingizwa nchini kuwa ni ‘Transit Sugarinayopitishwa nchini kwenda nchi za Burundi, Rwanda na Congo na kwamba baadhi ya wanatumia ujanja kuisambaza katika soko la Tanzania.
Uchunguzi uliofanywa na gazeti hili kwa kipindi cha mwezi mmoja sasa, umebaini kuwepo kwa ongezeko la sukari inayoingizwa nchini ambayo ni zaidi ya tani 200,000 katika kipindi cha miaka miwili iliyopita.
Chanzo: Tanzania Daima

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Kilimanjaro Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa