Home » » TFDA yaombwa kukagua pombe za kienyeji

TFDA yaombwa kukagua pombe za kienyeji


MAMLAKA ya Chakula na Dawa Nchini (TFDA) imeombwa kutanua wigo wa kufanya shughuli zake za ukaguzi hadi kwa watengenezaji wa pombe za kienyeji katika mikoa ya Kilimanjaro na Arusha ili kupunguza madhara mbalimbali yanayowapata watumiaji.
Mbali na ombi hilo pia serikali imeombwa kurasimisha vibali kwa watengezaji wa pombe za kienyeji katika mikoa hiyo ili kujiongezea kipato sanjari na kupunguza malalamiko toka kwa wazalishaji wengine wa vileo wanaofuata sheria kuchafuliwa katika soko.
Akizungumza wakati wa mkutano wa mawakala wa kampuni ya Banana Investment ya jijini Arusha, mkurugenzi wa kampuni hiyo, Adolf Olomi, alisema asilimia 90 ya watengezaji pombe za kienyeji hawajathibitisha bidhaa zao TFDA hali inayochangia pia kuuza bidhaa zao kwa bei ya chini.
“Bidhaa yoyote kwa ajili ya kula ama kunywa ambayo imetengenezwa ndani au nje ya nchi lazima ithibitishwe na TFDA kabla ya kuruhusiwa kuuzwa katika soko la Tanzania, kwa watengenezaji wa pombe za kienyeji asilimia 90 hawajaenda kuthibitisha bidhaa zao,” alisema Olomi.
Alisema iwapo vyombo vya serikali vinahitaji kutunza afya ya wananchi ni wajibu wa vyombo husika kuwatafuta watengenezaji wa pombe za kienyeji wathibitishe kama zinastahili au la.
“Tunafahamu wengi wao si rasmi kwa sababu hawajajisajili katika vyombo husika kama vile vya kulipa kodi na leseni hivyo gharama zao za uendeshaji zinakuwa kidogo kutokana na kwamba hawalipi gharama zile stahiki kwa vyombo husika,” alisema Olomi.
Alisema kutokana na kutokuwa na gharama katika uzalishaji wao hupelekea kuuza bidhaa zao kwa bei ya chini hatua inayochangia kutokuwepo kwa ushindani sawa katika soko la bidhaa hizo kwa watengenezaji wengine wanaofuata sheria.
Olomi alisema kampuni yake iko kwenye mkakati wa kufanya operesheni ya kuwakamata watengenezaji wa pombe za kienyeji ambao wamekuwa wakitumia vifungashio vya kampuni hiyo zikiwemo nembo pamoja na makasha kuweka bidhaa hafifu.
“Tuna mpango wa kuwatumia Majembe Auction Mart kwa ajili ya kuwakamata wote wanaotengeneza pombe za kienyeji na kisha kuziweka katika chupa na makasha yetu kwa lengo la kuwaaminisha watumiaji wa kinywaji hicho kuwa ndicho halisi kutoka katika kiwanda cha Banana,” alisema Olomi.
Naye meneja masoko wa kampuni hiyo David Damian alisema Banana Investment imetoa zawadi kwa mawakala waliofanya vizuri katika mauzo mkoa wa Kilimanjaro.
Chanzo: Tanzania Daima

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Kilimanjaro Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa