Home » » Polisi yaendelea kuwasaka waliomchinja mwenyekiti wa Chadema

Polisi yaendelea kuwasaka waliomchinja mwenyekiti wa Chadema


Wakati  jeshi la polisi likiendelea kuwasaka watu waliomchinja  hadi kufa Mwenyekiti wa Chadema, Kata ya Usa River, Msafiri Mbwambo (32), marehemu anatarajiwa kusafirishwa nyumbani kwake Same, mkoani Kilimanjaro kwa  aziko baada ya kuagwa kwa heshima zote za chama katika uwanja wa mpira wa Ngusero, wilayani Arumeru.
Marehemu Mbwambo  ambaye ameacha mke na watoto watatu alichinjwa majira ya saa 3:00 usiku juzi na watu ambao hawafahamiki na  mwili wake ulikutwa umtelekezwa makaburini.
Katibu wa Chadema, wa Wilaya ya Arumeru, Totinan Ndonde, alisema jana kuwa shughuli ya kuuga mwili wa marehemu zitafanyika katika uwanja wa mpira wa Ngusero kuanzia saa 6 mchana na mwili utasafirishwa kwenda Same kwa maziko.




Alisema chama makao makuu kimemteua Mbunge wa Musoma Mjini Chadema), Vincent Nyerere, kuwakilisha chama katika shughuli hiyo na kwamba viongozi ote wa chama mkoa na wilaya wanatarajiwa pia kushiriki.
“Mauaji haya yameleta simanzi kubwa kwa chama, wanachama na watu wa Arusha kwa jumla…tumeona shughuli ya kutoa heshima ya mwisho kwa mwili wa marehemu tuifanyie kwenye uwanja wa Ngusero ili kuwapa nafasi watu
wengi waweze kutoa heshima zao, “ alisema.
Mauaji hayo yanadaiwa  kufanywa eneo la Mukidoma, huko Usa River, huku kukiwa na utata mkubwa kuhusu sababu ya mauaji hayo. Baadhi ya watu wanayahusisha na sababu za kisiasa.
Kwa mujibu wa mashuhuda, walidai kuwa kabla ya tukio hilo marehemu alikuwa na wenzake kwenye eneo la sterehe huku yeye akiwa hanywi cho chote, lakini ghafla alipigiwa simu na watu hao, wakidai kuwa kulikuwa na wanachama wa chama kimoja cha siasa wanataka kurudisha kadi zao cha chama na kujiunga na Chadema.
Lakini wengine wanadai kuwa marehemu alipigiwa simu na mtu anayemfahamu akimtaka aende kuchukua fedha zake alizokuwa  akimdai.
Kamanda Andengenye alisema polisi bado wanafanya uchunguzi kuhusiana na tukio na kwamba hadi sasa hakuna mtu anayeshikiliwa kuhusiana na tukio hilo.
CHANZO: NIPASHE

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Kilimanjaro Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa