Home » » KADA wa Chadema Mahakamani kwa kubaka.

KADA wa Chadema Mahakamani kwa kubaka.


Na Daniel Mjema
Kada huyo ndiye ambaye katika Uchaguzi Mkuu wa 2010 alichuana na Mbunge wa sasa wa Jimbo la Mwanga ambaye pia ni Waziri wa Maji, Profesa Jumanne Maghembe na kushika nafasi ya pili.

KADA maarufu wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), Shafii Yatera (40), ameuanza vibaya mwaka 2013 baada ya kusherehekea Mwaka Mpya akiwa Gereza Kuu la Karanga mjini Moshi.

Yatera alipandishwa kizimbani juzi mbele ya Hakimu mkazi, Sophia Masati
akikabiliwa na tuhuma za kumbaka msichana mwenye umri wa miaka 17 ambaye ni mwanafunzi wa Shule ya Sekondari Msasani.

Kada huyo ndiye ambaye katika Uchaguzi Mkuu wa 2010 alichuana na Mbunge wa sasa wa Jimbo la Mwanga ambaye pia ni Waziri wa Maji, Profesa Jumanne Maghembe na kushika nafasi ya pili.Akimsomea mashtaka yake, Wakili wa Serikali Kanda ya Moshi, Oscar Ngole alidai kuwa Novemba 1,2012, mshtakiwa alimwingilia kimwili mwanafunzi huyo wa Kidato cha Nne kinyume cha sheria.

Wakili huyo alidai kuwa kitendo alichokifanya mtuhumiwa huyo ni kinyume cha kifungu 130 (2) (e) na 131 cha kanuni ya adhabu sura ya 16, adhabu ya kosa hilo ni kifungo cha miaka 30 jela. Hata hivyo kada huyo wa Chadema ambaye ni mkazi wa Pasua mjini Moshi alikanusha mashtaka hayo lakini upande wa mashtaka ukaiomba mahakama kuzuia dhamana kwa sababu za kiupelelezi.

Wakili Ngole, alidai kuwa endapo mshtakiwa atakuwa nje kwa dhamana ataathiri uchunguzi wa kesi hiyo kwa kile kinachodaiwa amekuwa akimshawishi mwanafunzi huyo kutokutoa ushirikiano kwa polisi.

Hakimu Masati anayeisikiliza kesi hiyo alilikubali ombi hilo la upande wa mashtaka na kuamuru mshtakiwa apelekwe rumande katika Gereza Kuu la Karanga hadi Januari 14, 2013 kesi hiyo itakapotajwa tena.

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Kilimanjaro Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa