Home » » ‘Wanaume wanaficha ukatili wa kijinsia’

‘Wanaume wanaficha ukatili wa kijinsia’

IMEBAINIKA wanaume wengi wanaofanyiwa vitendo vya ukatili na wake zao wanashindwa kuweka wazi vitendo hivyo kwa kuona aibu.
Hayo yalibainishwa juzi na Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Kanda ya Moshi, Aisha Nyerere, kwenye uzinduzi wa Siku 16 za kupinga ukatili wa kijinsia Kanda ya Kaskazini.
Alisema licha ya kuwa vitendo vya ukatili vimekuwa zaidi kwa wanawake na watoto lakini nao wanaume kwa sasa wanakabiliwa na vitendo hivyo.
“Naomba siku 16 za kupinga ukatili zitumike ipasavyo na hususan watu wote wanaohudhuria kampeni hizi kama unaona kuna mwanamume jirani yako anafanyiwa vitendo vya ukatili unaweza kumsaidia au mtu mwingine yeyote ili kutoa taarifa,” alisema.
Alisema vitendo vya ukatili wa kijinsia ambavyo bado vimeendelea kushika kasi ni pamoja na mauaji ya wivu wa kimapenzi, ukeketaji, mauaji ya vikongwe, rushwa ya ngono makazini, wajane, unyanyasaji majumbani na makazini.
Mratibu wa shirika lisilo la kiserikali linalopinga masuala ya ukeketaji kwa mwanamke (NAFGEM), Francis Selasini, alisema bado wanawake wanaongoza kwa kufanyiwa vitendo vya ukatili, lakini pia mitandao kwa sasa imeanza kupokea taarifa za wanaume wanaofanyiwa vitendo hivyo.
Mwenyekiti wa kamati ya maandalizi ya maadhimisho hayo Kanda ya Kaskazini, Elizabeth Mushi, alisema watazitumia siku hizo kutoa elimu, kuhamasisha watu na kutoa msaada wa kisheria
Chanzo;Tanzania Daima



0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Kilimanjaro Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa