Home » » MAGHEMBE AKATAA TAARIFA YA MHANDISI

MAGHEMBE AKATAA TAARIFA YA MHANDISI

WAZIRI wa Maji, Profesa Jumanne MaghembeWAZIRI wa Maji, Profesa Jumanne Maghembe, ameikataa taarifa ya hali ya utoaji wa huduma ya maji kwa Mkoa wa Kilimanjaro iliyosomwa na Mhandisi wa Maji wa mkoa huo, Immaculate Rafael, kutokana na kujaa makosa.
Waziri Maghembe alikuwa akipokea taarifa ya hali ya huduma ya maji kwa mkoa huo pamoja na kufanya ziara ya kuzindua upatikanaji wa maji katika Kata ya Kiboriloni  na Ngambo maeneo ambayo yalikuwa yakikabiliwa na tatizo la ukosefu wa huduma hiyo kwa kipindi kirefu.
Taarifa hiyo ilishindwa kuonyesha takwimu za kila wilaya na idadi ya watu wanaopata maji na  kwa asilimia gani, hatua iliyomlazimu Profesa Maghembe kusema kuwa njia iliyotumika kukokotoa takwimu hizo si sahihi.
“Nimesimama kueleza kuwa taarifa ya huduma niliyosomewa na mhandisi nilikuwa naifuatilia na kugundua kuwa ina makosa kwenye takwimu zilizopo na makosa hayo yametokana na njia iliyotumika kukokotolea takwimu hizo ambazo si sahihi, ” alisema.
Alisema kuwa uandaaji wa takwimu hizo ulikuwa na kasoro mbili; moja ikiwa ni jinsi ya kukokotoa pamoja na kuunganisha idadi ya watu wanaopatiwa maji maeneo ya mjini na maeneo ya vijijjni, jambo ambalo si sahihi.
Maghembe alisema kuwa katika kutafuta wastani wa wananchi wanaopata huduma ya maji lazima takwimu zionyeshe uhalisia wa watu wanaopata maji kulingana na wilaya na maeneo husika.
“Katika kutafuta wastani wa wilaya ambazo watu wake wanapatiwa maji huwezi kuchukua Wilaya ya Siha ambayo upatikanaji wake wa maji ni asilimia 80, Mwanga asilimia 68 na Moshi asilimia 75 ukajumlisha na kupata uhalisia wa watu wanaopata hiyo huduma,” alisema.
Hata hivyo alimtaka mhandisi huyo kusahihisha taarifa hiyo ili kupata takwimu halisi zenye kuonyesha wastani wa watu wanaopatiwa huduma hiyo.
Akitolea mfano Wilaya ya Rombo ambapo kuna mabonde na makorongo, alisema ni vema kuweka utaratibu utakaowawezesha kupata hesabu sahihi za wananchi wanaopata huduma hiyo.
Alisema katika lengo la taifa la upatikanaji wa maji na malengo la milenia ya serikali ni kuhakikisha kuwa huduma ya maji mijini inapatikana kwa asilimia 95 ifikapo mwaka 2015.
ChanzoTanzania Daima

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Kilimanjaro Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa