Home » » Wagonjwa KCMC hatarini

Wagonjwa KCMC hatarini

WAGONJWA wanaotibiwa katika Hospitali ya Rufaa ya KCMC, watumishi na wageni wanaowauguza wagonjwa, afya zao zipo hatarini kutokana na kukumbwa na magonjwa ya mlipuko na maji wanayotumia katika hospitali hiyo kudaiwa si safi na salama.
Uchunguzi uliofanywa na Tanzania Daima umebaini taarifa za maji yanayotumiwa kwenye hospitali hiyo kudaiwa kuwa  na dalili za uchafu (contaminated), iliyoibuliwa na mmoja wa madaktari (jina tunalo) kwenye kikao kilichokaa Januari 8, mwaka huu baada ya kuyafanyia maji hayo utafiti.
Awali Hospitali ya Rufaa ya KCMC ilikuwa ikitumia maji ya kwenye tanki ambayo yalikuwa yakiwekwa dawa, lakini matumizi ya maji yalipokuwa mengi ililazimu kuyafungulia maji hayo kuingia kwenye mzunguko moja kwa moja kutoka kwenye visima.
Mkurugenzi wa huduma wa hospitali hiyo, Profesa Raimos Olomi, ambaye pia alikuwa akikaimu nafasi ya Mkurugenzi wa Hospitali, alikiri kuwepo kwa tatizo hilo huku akisema walishafanya utafiti wa awali lakini wanasubiri matokeo kutoka mamlaka ya maji.
“Ni kweli tatizo hilo lipo maji kudaiwa ni dalili za uchafu (contaminated) lakini tunasubiri majibu ya mamlaka na tatizo si kubwa kwa sababu kuna maeneo mengine maji ni safi na salama lakini maeneo mengine yameonekana kuwa na tatizo,” alisema.
Taarifa za ndani zilieleza kuwa huenda tatizo hilo la maji kuwa machafu linaweza likawa limesababishwa na moja ya visima vinavyotumiwa na hospitali hiyo kutofanyiwa usafi kwa muda mrefu.
Watumishi waliozungumza na Tanzania Daima walisema uongozi haujachukua hatua za haraka tangu tatizo hilo la maji lilipogundulika, hali ambayo inashusha hadhi ya hospitali hiyo inayotegemewa nchi nzima pamoja na nje ya nchi.
Kwa upande wa kisima kuwa ndiyo sababu ya maji hayo kuwa machafu kutokana na kutofanyiwa usafi, alisema kama ingekuwa chanzo cha maji wanayotumia ndiyo inapelekea maji hayo kuwa machafu basi maeneo yote maji yangeonekana machafu, hivyo si tatizo linalotokana na chanzo.
Hata hivyo kutokana na tatizo hilo hospitali hiyo imetoa tahadhari ambapo kuna wagonjwa, watumishi na wageni wengine wanaowaangalia wagonjwa kulazimika kununua maji ya chupa madukani ili kuweza kuepukana na hali hiyo.
Chanzo;Tanzania Daima

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Kilimanjaro Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa