Home » » Polisi walaumiwa kuhoji watuhumiwa kwa nguvu

Polisi walaumiwa kuhoji watuhumiwa kwa nguvu

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 

Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kakusulo Sambo amewajia juu polisi kwa tabia yao ya kutumia nguvu na kukiuka sheria wanapochukua maelezo ya washtakiwa na kusababisha ushahidi muhimu kupotea.
Jaji Sambo alitoa kauli hiyo juzi wakati akitoa uamuzi mdogo katika kesi ya mauaji ya polisi wa Kikosi cha Kutuliza Ghasia (FFU), PC Michael Milanzi inayowakabili raia wawili wa Kenya na Watanzania 10.
Uamuzi huo ulitokana na pingamizi la mawakili wa utetezi baada ya upande wa mashtaka kuomba maelezo ya ungamo la mshtakiwa wa pili, Peter Kimani yapokelewe mahakamani kama kielelezo.
Maelezo hayo yalichukuliwa Agosti 13, 2007 na Hakimu wa Mahakama ya Mwanzo, Jumanne Shimbos baada ya mshtakiwa huyo kuomba apelekwe kwa mlinzi wa amani ili aweze kukiri makosa yake.
Mawakili wa Utetezi, Majura Magafu, Profesa Jonas Itemba, Faustine Matemu, Ralph Njau na Martin Kilasara walipinga maelezo hayo wakisema yalichukuliwa nje ya muda ulioidhinishwa kisheria.
Kwa mujibu wa mawakili hao, kifungu cha 50 na 51 cha Sheria ya Mwenendo wa Makosa ya Jinai (CPA), kinataka maelezo ya mtuhumiwa yachukuliwe ndani ya masaa manne tangu kukamatwa.
Endapo polisi anayechukua maelezo hayo ataona anahitaji kuendelea kumhoji mtuhumiwa, anapaswa kuomba kwa bosi wake na ombi hilo liandikwe kwenye maelezo. Hata hivyo, mawakili hao walisema maelezo ya ungamo ya mshtakiwa wa pili ambaye ni raia wa Kenya, yalichukuliwa na mlinzi wa amani siku 13 baada ya kukamatwa kwake Julai 20, 2013.
Wakili wa Serikali, Ladslaus Komanya anayeendesha kesi hiyo akisaidiwa na wakili Stella Majaliwa na Ignas Mwinuka, walisema vifungu hivyo havizungumzii maelezo ya ungamo kwa mlinzi wa amani.
Katika uamuzi wake mdogo, Jaji Sambo alikubaliana na hoja ya mawakili hao wa Serikali, lakini akasema ipo kesi ya mifano ya Mahakama ya Rufaa iliyojumuisha pia maelezo ya mlinzi wa amani.
Jaji Sambo aliwalaumu moja kwa moja polisi kuwa wanatumia nguvu wakati wa kuchukua maelezo ya mtuhumiwa anayekiri kosa badala ya kufuata maelezo ya vifungu hivyo vya CPA.
Kwa mujibu wa Jaji Sambo, dosari hizo zinazofanywa na polisi zinawapa shida mawakili wa Serikali kutetea hoja mahakamani na kufanya ushahidi muhimu kama huo kutochukuliwa na mahakama.
Chanzo;Mwananchi

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Kilimanjaro Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa