Home » » Baba adaiwa kuishi kinyumba na binti zake

Baba adaiwa kuishi kinyumba na binti zake

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 

Mkazi mmoja wa Same mkoani Kilimanjaro anashikiliwa na polisi kwa tuhuma za kuwabaka watoto wake wawili kwa kipindi cha miaka minne mfululizo.
Mwanamume huyo anatuhumiwa kuwageuza watoto hao wake zake tangu alipoachana na mkewe mwaka 2010.
Bibi wa watoto hao, Joyce Mmbaga alisema taarifa za ukatili huo alizipata kwa mmoja wa wajukuu zake hao ambaye kwa sasa ana umri wa miaka 14. Alimkariri mjukuu huyo akisema kwamba amekuwa akibakwa na baba yake mzazi tangu mwaka 2011 na kila anapomfanyia unyama huo alimtishia kumuua kama angemwambia mtu.
Mmbaga alisema siri hiyo ilivuja baada ya kuanza jitihada za kumtafutia shule mjukuu huyo ili arudie darasa la saba baada kushindwa kufaulu. Alisema mtoto huyo alimweleza kwamba hakuwa tayari kusoma shule za Same Mjini na kutaka kupelekwa mbali na mazingira ya nyumbani.
Bibi huyo alieleza kuwa alitii ombi la mjukuu wake na kumpeleka Kata ya Gonja ambako aliendelea na masomo lakini baba yake alikuwa akimpigia simu kupitia kwa mama anayeishi na mtoto huyo akitaka mtoto wake arudi nyumbani.
“Baba yao alidai mtoto arudi nyumbani na akaanza kumtukana mama aliyekuwa akiishi na huyu mtoto hali iliyomfanya mama huyo aanze mipango ya kumrudisha nyumbani kuepuka matusi ya baba yake. Lakini mtoto alivyosikia anarudishwa kwa baba yake alilia sana na kunyanyua Biblia juu akiomba Mungu amchukue ili aachane na maisha ya kuishi na baba yake,” alisema.
Alisema kilio kile kilimfanya mama huyo kukaa na mtoto huyo na kuanza kumhoji sababu ndipo alipodai kuwa baba yake amekuwa akifanya naye mapenzi yeye na mdogo wake tangu mama yao alipoondoka na kuwaacha.
Mmbaga alisema baada ya maelezo hayo walipiga simu polisi ambao waliwachukua watoto hao na kuwahoji kisha kuwapeleka Hospitali ya Same kwa uchunguzi.
Imeelezwa kwamba taarifa ya kidaktari ilionyesha kuwa watoto hao wamebakwa kwa muda mrefu kiasi cha kuharibu maumbile yao.
Kaimu Kamanda wa Polisi Mkoa wa Kilimanjaro, Koka Moita alisema jeshi lake linaendelea na uchunguzi na baba huyo atafikishwa mahakamani muda wowote uchunguzi utakapokamilika.
Chanzo;Mwananchi

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Kilimanjaro Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa