Home » » TTB YAMPA UBALOZI WA HESHIMA MMAREKANI

TTB YAMPA UBALOZI WA HESHIMA MMAREKANI

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 
Macon Dunnagan BODI ya Utalii Tanzania (TTB), imempa ubalozi wa heshima wa utalii nchini Marekani, Macon Dunnagan aliyeutangaza Mlima Kilimanjaro kwa miaka 35.
Akizungumza wakati wa kumpokea mtalii huyo aliyeupanda mlima Kilimanjaro kwa zaidi ya mara 35  katika geti la Marangu, Ofisa Uhusiano wa TTB, Augustina Makoye, alisema wameshawishika kumpa ubalozi wa heshima raia huyo ya Marekani, kutokana na juhudi zake za kuutangaza mlima huo mrefu kuliko yote barani Afrika.
“Dunnagan amekuwa akitembelea majimbo mbalimbali nchini Marekani, kwa ajili ya kushawishi na kuhamasisha watu kuupanda mlima Kilimanjaro kwa kujitolea bila malipo yoyote, hivyo TTB imeona ni vema kumpa heshima ya kuwa balozi wetu huko,” alisema Makoye.
Pia, Makoye alisema TTB kwa muda mrefu imekuwa haina wawakilishi wake katika majimbo nchini Marekani, hivyo kumpata Dunnagan ni mojawapo ya jambo muhimu katika kukuza sekta ya utalii hapa nchini kwa mataifa mbalimbali.
Kwa upande wake, Dunnagan aliishukuru serikali ya Tanzania kwa kuutambua mchango wake katika kukuza utalii wa nje na kuongeza kwamba, huo ni mwanzo tu ataendelea kutoa ushawishi kwa watu wa Marekani kuzuru Mlima Kilimanjaro.
Itakumbukwa kwamba Macon aliongozana na watalii tisa kutoka katika klabu za ‘rotary’ nchini Marekani wakiwa na madhumuni ya kuchangisha fedha kwa ajili ya mapambano dhidi ya Polio.
Dunnagan na wenzake, walifanikiwa kuchangisha sh milioni 480 takribani dola 300,000 za Marekani, ambazo zimetolewa kwa ajili ya kuwafikia watoto wenye matatizo hayo.
Naye Mhifadhi Mkuu wa Hifadhi ya Mlima Kilimanjaro (Kinapa), Erastus Lufungulo, alisema watalii wengi kutoka Marekani wamekuwa wakizuru kivutio hicho kutokana na hamasa ya Dunnagan na kwamba, sekta ya utalii imeendelea kukua hapa nchini kutokana na wageni wengi kutembelea vivutio.
Chanzo:Tanzania Daima

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Kilimanjaro Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa