Home » » CHADEMA NI ‘AMSHA AMSHA’

CHADEMA NI ‘AMSHA AMSHA’

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 
Mwenyekiti wa Kanda ya Pwani Chadema, Mabere Marando akikata utepe kuzindua Bendi ya Wanawake na Operesheni Amsha Wanawake Tanzania katika viwanja vya Tanganyika Packers Kawe Dar es Salaam jana. Bendi hiyo itatumika kuhamasisha katika mikutano ya Ukawa.
 
Chadema imefanya mikutano mikubwa ya kuamsha wapigakura katika mikoa ya Kilimanjaro, Manyara, Dar es Salaam na Tanga huku mwenyekiti wake, Freeman Mbowe akisema mawaziri wa Rais Jakaya Kikwete waliotangaza nia ya kugombea urais ‘wanaivua nguo’ Serikali waliyomo kwa kueleza maovu ya ndani.
Alisema mawaziri hao hawana sauti moja, kila mmoja anazungumza lake kuikosoa Serikali kwa kuahidi kufanya mambo mazuri tofauti na yale yanayofanywa na Serikali ya sasa ya Kikwete.
Hadi sasa makada 38 wa CCM wamechukua fomu za kuomba kuwania urais, miongoni mwao wakiwamo Makamu wa Rais, Dk Mohamed Gharib Bilal, Waziri Mkuu, Mizengo Pinda, mawaziri 10 na naibu mawaziri wawili.
Katika kutangaza sifa zao baadhi yao wamekuwa wakijigamba watatatua kero za ufisadi, migogoro ya ardhi, kudorora kwa uchumi na kuporomoka kwa thamani ya shilingi.
Akizungumza na Mwananchi jana, Mbowe alisema Chadema haiwezi kuiga mfumo huo kwa sababu wana utaratibu wao wa kutangaza nia na kuchukua fomu.
Alisema ratiba yao ya kuchukua fomu za urais ilishatolewa na itaanzia Julai 20 hadi Julai 25, mwaka huu.
“Mawaziri wa Kikwete hawana sera, wamesahau kuwa nao ni sehemu ya serikali hiyo iyo wanayoikosoa. Chadema tuna utaratibu wetu wa kutangaza nia na kuchukua fomu, nafasi ziko wazi,” alisema Mbowe.
Alipoulizwa wamefikia wapi kuhusu mgombea atakayewakilisha vyama vinavyounda Ukawa, Mbowe alisema bado wanafanya mashauriano, muda wowote wakimaliza mgombea wa Ukawa atatangazwa.
“Hii ni vita, hatuwezi kumweka wazi mgombea wetu kwa sababu bado ni mapema. Ukawa bado tunafanya consultations (mashauriano), tukimaliza Watanzania watamjua mgombea wa Ukawa,” alifafanua kiongozi huyo.
Mbowe alipuuza madai kuwa Ukawa inavunjika, akisema haiwezi kuvunjika kama watu wanavyodhani hasa baada ya Mwenyekiti wa Chama cha Wananchi (CUF), Profesa Ibrahim Lipumba kuchukua fomu ya kuwania urais ndani ya chama chake.
Alisisitiza kuwa Ukawa haijazuia chama chochote kuchagua mgombea urais kama walivyofanya CUF bali chama chochote kitasimamisha mgombea wake kisha wagombea wote kushindanishwa na kumpata mmoja wa Ukawa.
“Jambo hili tuliliweka wazi tangu awali, kusimamisha mgombea wa chama siyo hatua ya mwisho, ni sehemu ya mchakato wa kumpata mgombea wa Ukawa,” alisema Mbowe.
Hata hivyo, Mbowe hakuweka wazi tarehe ya kutangazwa kwa mgombea wa Ukawa kwa madai kwamba mashauriano yanaendelea.
Ataka mashine za BVR zizuiwe
Akiwa mkoani Kilimanjaro, Mbowe amewataka wananchi kuzuia mashine za BVR endapo hadi kufikia leo kutakuwa na watu wengi ambao hawajaandikishwa kwenye Daftari la Wapigakura.
Mbowe alisema hayo juzi jioni katika mkutano wa hadhara uliofanyika Kijiji cha Shirimatunda.
“Kujiandikisha kwenye BVR ni haki na wajibu wa kila Mtanzania. Yapo maeneo mashine ni chache. Ikifika kesho (leo) mfanye tathmini ya idadi ambao hawajaandikishwa,” alisema Mbowe na kuongeza;
“Ikiwa kutakuwepo na watu wengi hawajaandikishwa basi mhakikishe haiondoki mashine hata moja hadi watu wote waandikishwe kwa sababu hizi mashine zimenunuliwa kwa kodi zenu na si fadhila”.
Hata hivyo, Mbowe aliwataka viongozi wa kata zitakazokuwa na idadi kubwa ya watu ambao hawajaandikishwa, wawasilishe malalamiko mapema kwenye Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC).
“Kabla ya kufikia hatua hiyo mhakikishe mmepeleka malalamiko NEC. Aliyetenga siku saba za kujiandikisha ni mwanadamu na ni huyo huyo anayeweza kuongeza siku,” alisisitiza Mbowe.
Amsha Wanawake Dar
Awali akizungumza katika uzinduzi wa mkakati wa Amsha Wanawake kwa ajili ya Uchaguzi Mkuu Dar es Salaam jana, Mjumbe wa Kamati Kuu, Mabere Marando aliwataka makada wa vyama vya Ukawa kuacha hofu juu ya hatima ya umoja huo kwa kuwa bado upo imara na haujatetereka.
Alisema amekuwa akisikia kuwapo kwa “uoga uoga juu ya msimamo wa Ukawa…kuna uvumi uvumi unaendelea baada ya juzi mhemishiwa Profesa Lipumba kuchukua fomu... ule ni urataratibu wa kawaida ambao viongozi wa juu wa Ukawa walikubaliana kuwa kila chama kifuate taratibu za chama hicho hata Chadema tutafanya hivyo, NLD, CUF na NCCR-Mageuzi,” alisema.
“Ukawa ipo imara…mimi nipo katika ngazi za juu za maamuzi, hatujatetereka, tutawapa Watanzania mgombea mmoja wa kiti cha urais, mmoja udiwani na ubunge…hakuna kitakachobadilika, Watanzania msiwe na wasiwasi,” alisema Marando huku akishangiliwa.

Wabunge washambulia Manyara
Katika hatua nyingine, wabunge saba wa Chadema na mmoja wa NCCR-Mageuzi jana waliushambulia Mkoa wa Manyara na kuendesha mikutano ya hadhara kwa lengo la kuhamasiha wananchi wajiandikishe kwenye BVR.
Wabunge hao ni Joseph Selasini (Rombo), Rose Kamili, Pauline Gekul, Joyce Mukya, Cecilia Pareso , Grace Kiwelu (wote viti maalumu) na Mbunge wa NCCR Kasulu Mjini, Mosses Machali.
Wabunge hao ambao awali walikuwa katika mikoa ya Kilimanjaro na Arusha jana walitembelea kata za Maskta, Endasak, Maeskroni na Mingenyi na mbali ya kuhamasisha wananchi wajiandikishe waliwataka waiondoe CCM ifikapo Oktoba.
Akizungumza katika mikutano hiyo, Kiwelu aliwataka wananchi wa eneo hilo kumchagua mbunge wa Chadema kwani ndiye atakayeweza kuwaletea maendeleo.
“Nawapa pole wananchi wa Hanang’ kwani mlipata viongozi wakubwa kama Frederick Sumaye aliyekuwa waziri mkuu kwa vipindi viwili lakini hakuna hata barabara kwenye jimbo lenu kwani njia wanayopitia ng’ombe ninyi ndiyo mnapita,” alisema Kiwelu na kuongeza.
“Tumepita kwenye barabara ambayo wanapita ng’ombe na maji mnayotumia siyo safi wala salama, kwetu Kilimanjaro kuna huduma bora ikiwamo ya umeme, hospitali na maji kutokana na wananchi kuichagua Chadema.”
Kwa upande wake, Gekul alisema wananchi wa mkoa wa Manyara, wamechoshwa na CCM hivyo wamejipanga kikamilifu kuhakikisha wanaiangusha Oktoba.
“Hatutaiondoa CCM kwa rungu wala fimbo ila tutaiondoa kwa kutumia kura za wananchi, nawaomba wananchi wote kama mna hasira kutokana na huduma mbovu zinazotolewa na CCM ichagueni Chadema,” alisema Gekul.
Mbunge wa Rombo, Joseph Selasini aliwataka wakazi wa eneo hilo kutomchagua tena mbunge wa jimbo hilo, Mary Nagu kwa kuwa ameshindwa kuwaletea maendeleo japokuwa amekuwa waziri kwa kipindi kirefu.
“Mimi nimetokea Mkoa wa Kilimanjaro na kule kuna maendeleo mengi na huduma za kijamii na barabara za lami yeye Nagu amekuwa mbunge wenu kwa miaka kumi lakini ameshindwa kuwaleta hata maji,” alisema Selasini.
Machali aliwataka wananchi wa jimbo hilo kuchagua wagombea wa Ukawa ili wapate maendeleo kwa kuwa licha ya Hanang’ kuwa eneo zuri lenye rutuba na mifugo mingi lakini wananchi wake wanaishi kwenye lindi la umaskini.
“Hakuna sababu ya kuendelea kuichagua CCM kama wameshindwa kuleta maendeleo, hivyo ninyi wenyewe ndiyo mnao maamuzi ya ama kuendelea kunyonywa kwa miaka yote au kupata ukombozi kwa kuchagua Ukawa,” alisema Machali.
Mwalimu na vyuo vikuu
Naibu katibu mkuu wa chama hicho (Zanzibar), Salum Mwalimu amewakumbusha vijana wa vyuo vikuu kusimamia kupatikana kile alichokiita uhuru wa pili wa nchi wenye lengo la kuwakomboa Watanzania kutoka maisha magumu.
Mwalimu aliyasema hayo jana mjini Lushoto wakati akiongoza mahafali ya wanafunzi wanachama wa Chadema wa Chuo Kikuu cha Kumbukumbu ya Sebastian Kolowa (Sekomu) alikokabidhi vyeti kwa wahitimu.
Mwalimu alisema kuna ushawishi mkubwa unaofanywa na CCM kwa wanafunzi wa vyuo vikuu kwa kumwaga fedha na ahadi za vyeo na ajira ili kuwapumbaza vijana kuondoka katika mstari wa harakati. Alisema Serikali ya Ukawa itatatua changamoto zilizopo elimu ya juu katika kipindi cha kwanza cha miaka mitano.
Chanzo:Mwnanchi

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Kilimanjaro Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa