Home » » KAVAZI LA MWALIMU NYERERE NI HAZINA YA FALSAFA KWA WATANZANIA.

KAVAZI LA MWALIMU NYERERE NI HAZINA YA FALSAFA KWA WATANZANIA.


     Na Jovina Bujulu-MAELEZO
Ni miaka 17 tangu Mwalimu Julius Kambarage Nyerere afariki dunia. Ingawa amefariki lakini fikra zake bado zinaishi kama alivyowahi kusema mwanazuoni mmoja Seneta wa zamani wa Arkansas Bruce Holland “viongozi mahiri hawafi wanaishi milele kupitia fikra zao na maisha yao”.

Kwa kuenzi mchango wa Mwalimu Nyerere kupitia fikra zake mnamo mwaka 2012 watatafiti watatu walibuni wazo la kufanya utafiti kuhusu fikra na falsafa za Mwalimu Nyerere, Wanazuoni hao ni Profesa Issa Shivji, Profesa Saida Yahaya Othman na Dkt. Ng’anzi Kamata.

Wanazuoni hao walihitimisha utafiti huo kwa kuandika bayografia ya Mwalimu Nyerere ambapo walianzisha kavazi la Mwalimu Nyerere ambalo ni kituo huru kilichoanzishwa mwaka 2014 ndani ya Tume ya Taifa ya Sayansi na Teknolojia (COSTECH). Kavazi hilo lilizinduliwa mwaka 2015 na Rais Mstaafu wa awamu ya tatu Mhe. Benjamin William Mkapa.

Akizungumzia utafiti wa Bayografia (Wasifu) ya Mwalimu Nyerere, Dkt Bashir Ally ambaye ni mjumbe wa kamati ya utendaji ya Kavazi hilo alisema kuwa ingawa watu mbali mbali wameandika bayografia ya Mwalimu Nyerere, utafiti uliofanywa na wanazuoni hao watatu ni wa kwanza na wa kipekee uliofanywa kwa kina tofauti na Bayografia za watu wengine.

Dkt. Bashir anaendelea kusema kwamba wanazuoni hao wanaendelea kukusanya taarifa mbali mbali za Mwalimu Nyerere, na nyaraka nyingi kutoka vyanzo mbali mbali na kuzihifadhi katika Kavazi.

“Taarifa za nyaraka zinazohusu kazi na maisha ya Mwalimu zinazopewa uhai kwa kujadiliwa na kudadisiwa na watafiti wengine ndani na nje ya nchi hasa vijana kwa sababu zinabeba historia ya nchi”. anaongeza Dkt. Bashir.

Kavazi la Mwalimu Nyerere limetafsiriwa kama ni mahali maalumu ambapo kumbukumbu za machapisho ya Mwalimu zimekusanywa na watafiti na kuhifadhi pamoja. Kavazi hilo  linatoa fursa kwa watafiti kubuni fikra mpya zenye misingi ya fikra za Mwalimu Nyerere.

Fikra hizo zinatumika kama nyenzo muhimu katika kufanya utafiti za kisayansi zitakazowezazesha nchi kupiga hatua za maendeleo kiuchumi kwa kuongeza ubunifu katika rasilimali kwa lengo la kuwanufaisha wananchi wote.

Kavazi la Mwalimu ambalo linatumika kama kituo cha kuhifadhia na kuzipa uhai fikra  zake limekwisha chapishwa machapisho matatu na mijadala mbalimbali.

Machapisho hayo ni ushairi ambao Mwalimu Nyerere   aliouandika katika miaka ya 1950 na 1960, uanazuoni wa Mwalimu na insha tatu za kifalsafa na mjadala wa Pan-African Nationalist or Nationalist Pan-Africa.

Aidha, Kavazi la Mwalimu limefanya Mhadhara tarehe 28, mwezi Septemba, 2016 ambapo mgeni rasmi alikuwa Mhe. Joseph Warioba ambaye ni Waziri  Mkuu Mstaafu.

Mhadhara huo ulihusu elimu ya juu katika maendeleo ya Afrika na uliambatana  na ufunguzi wa hifadhi ya Nyaraka ya Mwalimu Nyerere na uzinduzi wa chapisho la 4 la kavazi.

Akizungumzia shughuli za Kavazi la Mwalimu Dkt. Bashir anasema kwamba ni pamoja na kuhifadhi nyaraka zilizokusanywa na waandishi wa bayografia ya Mwalimu Nyerere ili zitumiwe na watafiti, kutoa nafasi ya mjadala ya kizuoni na kimkakati juu ya masuala muhimu ya maendeleo ya jamii, na kuandaa na kuendesha mafunzo ya nadharia na mbinu za utafiti wa masuala ya maendeleo ya jamii.

Aidha, Dkt. Bashir anasema kwamba Kavazi la Mwalimu linatoa mafunzo kwa wanazuoni na wasomi chipukizi waliopo kwenye taasisi za elimu ya juu na asasi zisizo za kiserikali.

“Kavazi limekwishafanya mafunzo kwa vijana ambayo yaliangalia rasilimali, dhana, na nadharia mbalimbali na mbinu za kiutafiti ambazo zinawapa maarifa na uwezo wa kuendeleza utafiti”. Anasema Dkt Bashir.

Wafadhili wa Kavazi la Mwalimu ni pamoja na Shirika la Taifa la Hifadhi ya Jamii (NSSF) ambao walichangia fedha za awali, Taasisi ya Kijerumani ya Rossa Luxemburg na watu mbalimbali.
Kavazi la Mwalimu limeanzisha mfuko maalumu (Endoworment Fund) ambao utazalisha fedha za kujiendesha, hata hivyo wananchi wanaombwa kuendelea kujitokeza kuchangia mfuko huo ili kukuza na kuendeleza kazi za Kavazi.

Akizungumzia mapokeo ya Kavazi la Mwalimu Dkt. Bashir anasema ni mazuri kwa sababu viongozi mbalimbali wamekwisha tembelea Kavazi hilo wakiwemo Marais Wastaafu Mhe. Benjamini Mkapa, Mhe. Ally Hassan Mwinyi na Mkurugenzi wa Taasisi ya Mwalimu Nyerere,  Mzee Joseph Butiku na ujumbe wake.

Viongozi wengine waliotembelea Kavazi hilo ni pamoja na Mawaziri Wakuu  wastaafu Mhe Cleopa David Msuya, Jaji Joseph Sinde Warioba, Dkt Salim Ahmed Salim na wanasiasa mbalimbali wakiwemo waliofanya kazi na Mwalimu Nyerere ambao ni Mze Geroge Kahama na Mzee Kingunge Ngombale Mwiru familia ya Mwalimu Nyerere pamoja na wananchi mbalimbali.

Alisifu ushirikiano wanaoupata kutoka Makumbusho ya Taifa, Taasisi ya Mwalimu Nyerere na baadhi ya vyombo vya habari kuwa umewawezesha kufanya kazi yao kwa ufanisi, hasa kukusanya nyaraka na taarifa za Mwalimu Nyerere.

Naye Mkurugenzi wa Kavazi la Mwalimu, Profesa Issa Shivji ametoa wito kwa viongozi na wanasiasa mbalimbali waliofanya kazi na Mwalimu Nyerere kupeleka nyaraka zao katika Kavazi kwajili ya kuhifadhiwa na kufanyiwa tafiti mbali mbali.

Dkt. Bashir anamalizia kwa kuwakaribisha wananchi kutembelea Kavazi ili kujisomea nyaraka na kazi za Mwalimu  na kufahamu historia ya nchi yetu. Aidha anasema kuwa hakuna tozo yoyote kwa wananchi wanaokwenda kutembelea Kavazi hilo. 
 
Ama kweli Mwalimu Nyerere alikuwa Mwanafalsafa hodari na makini sana ambaye mawazo au falsafa zake zitakumbukwa vizazi hadi vizazi hasa suala la kutetea wanyonge, usawa wa binadamu na upendo kwa wote bila kujali itikadi, dini wala kabila la mtu.

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Kilimanjaro Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa