Home » » Sumaye 'atema cheche' Marekani

Sumaye 'atema cheche' Marekani


WAZIRI Mkuu mstaafu, Bw. Frederick Sumaye, juzi aliongoza mhadhara unaohusu maendeleo ya Bara la Afrika katika Chuo Kikuu cha Columbus, jijini New York, nchini Marekani.

Katika mhadhara huo, Bw. Sumaye alichambua kwa kina masuala mbalimbali yanayopaswa kupewa kipaumbele ili kuharakisha maendeleo barani Afrika.

Hatua ya Bw. Sumaye kuongoza mjadala katika mhadhara huo wa Kimataifa, inatafsiriwa ni moja ya kazi zinazochukuliwa na makada wanaotajwa kutaka kugombea urais kama njia moja wapo ya kujiongezea sifa kitaifa na kimataifa.

Wakati Bw. Sumaye akiibukia nchini humo, wanasiasa wengine wanaotajwa katika kinyang'anyiro hicho wamekuwa wakishiriki shughuli mbalimbali za kijamii nchini na kutoa misaada.

Hiyo ni safari ya pili kwa Bw. Sumaye kualikwa kutoa mihadhara kwenye vyuo vikuu mbalimbali nchini Marekani ambapo awali alifanya ziara kama hiyo na kutoa mhadhara katika vyuo vikuu kikiwemo Chuo Kikuu cha Harvard, alikosomea.

Hatua ya kualikwa mara kwa mara katika vyuo vilivyopo katika nchi za Magharibi, inaonesha huenda kuna uungwaji mkono kwa namna moja ama nyingine kutoka nchi hizo.

Bw. Sumaye alisema, nchi za Afrika zinatakiwa kujipanga upya na kuongeza ushirikiano ili kutumia zaidi masoko ya ndani badala kutegemea masoko ya nje yenye ushindani mkubwa na ukatili.

Alisema nchi nyingi za Afrika zimekuwa zikifanya biashara zaidi na nchi za Magharibi au Mashariki lakini zimekuwa zikikosa ushindani kutokana na kuwekewa vikwazo mbalimbali hususan viwango vya ubora na ujanja mwingine.

"Kama nilivyosema awali, ugawaji uliofanywa na wakoloni, kuzigawa nchi za Afrika katika mataifa madogo kulisababisha madhara makubwa mawili katika uchumi wa bara  hili.

"Moja ni kuendelea na utegemezi kwa wakoloni wa zamani, pili ni udhaifu kutokana na udogo wa nchi," alisema Bw. Sumaye na kuongeza kuwa, ili kuondokana na matatizo hayo  nchi za Afrika lazima zijenge msingi wake imara na kufanya kazi kwa pamoja kuanzia eneo hilo.

Aliongeza kuwa, nchi za Afrika lazima zijitambue kuwa ni dhaifu sana katika masuala ya kiuchumi akisema umefika wakati wa kuunda umoja wao ambao utakuwa na nguvu ya kuinua uchumi wa nchi hizo.

Bw. Sumaye alisema, kama nchi hizo zitafanikiwa kujiunda katika makundi ya kikanda, itazisaidia kuwa na sauti ya pamoja katika kuimarisha uchumi wake.

"Nchi nyingi za Afrika zinashindwa kufanya biashara zaidi na nchi za Magharibi au Mashariki kutokana na vikwazo vya ubora wa bidhaa wanavyowekewa," alisema.

Aliongeza kuwa, nchi hizo zina uwezo mkubwa wa kuzalisha bidhaa nyingi zinazoweza kuleta ushindani katika masoko ya kisasa duniani ambapo upangaji upya katika makundi ya kiuchumi kama ECOWAS, Jumuiya ya Afrika Mashariki-EAC, SADC, COMESA, unaweza kuwa jambo muhimu katika kuimarisha uchumi wa Afrika.

Alishauri sekta binafsi ilindwe na ipewe umuhimu unaostahili na kulinda viwanda vichanga ambapo akizungumzia sera za uwekezaji, alishauri ziangaliwe upya ili ziwalinde wawekezaji, kulinda masilahi ya nchi na wananchi kwani baadhi ya sera hizo zimewekwa kutokana na ushawishi wa wakubwa kwa masilahi yao.

Upande wa elimu, alisema usomi ni pamoja na kujitoa mhanga kwa ajili ya wengine, kuwa na uzalendo wa kweli ambapo wasomi
wasitumike kuondoa uchumi mbovu na umaskini hivyo lazima  Afrika ikubali mabadiliko ya fikra. 

Chanzo Gazeti la Mwananchi.



Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399.

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Kilimanjaro Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa