Home » » MOSHI WATOFAUTIANA MVUTANO RC, MADIWANI

MOSHI WATOFAUTIANA MVUTANO RC, MADIWANI

na Rodrick Mushi, Moshi
WAKAZI wa Manispaa ya Moshi wametofautiana kuhusu mvutano uliopo baina ya Mkuu wa Mkoa wa Kilimanajro, Leonidas Gama, na Baraza la Madiwani wa Manispaa ya Moshi linaloongozwa na CHADEMA.
Mvutano huo ni ule wa mkuu wa mkoa kuzuia safari ya madiwani na watendaji kwenda Kigali, Rwanda.
Wakizungumza kwa nyakati tofauti jana, baadhi ya wananchi walisema hawahitaji mvutano wa kisiasa kwani kama mkuu wa mkoa ingependeza zaidi wakashauriana kwa lengo la kuleta maendeleo na sio kujitafutia umaarufu kupitia vyombo vya habari.
“Ukifuatilia utagundua mkuu wa mkoa ana makosa, kwani kulikuwa kuna ubaya gani kama wangekaa wakashauriana na kama anasema wangetumia sh milioni 200 basi angeacha waende ndipo awashtaki kwa wananchi maana sisi ndio tuliowachagua,” alisema Peter Anase, mkazi wa kata ya Njoro.
Alisema kinachoonekana ni kutaka kudhoofisha baraza la madiwani ambalo linaongozwa na upinzani, hivyo ni vema serikali ya CCM ikawaacha madiwani hao wakafanya kazi na kama wakishindwa basi wahukumiwe kwenye uchaguzi na wananchi.
Lakini kwa upande mwingine, wapo wananchi waliohoji kuhusiana na ahadi ambazo walitoa madiwani wakati wa kampeni mwaka 2010 kuwa ni kuondoa safari zote ambazo si za lazima za madiwani na watendaji kwenda nje ya nchi.
Mmoja wa wananchi ambao hawakutaka kutaja majina gazetini alisema fedha ambazo zilikuwa zitumike kwenye safari hiyo ni kubwa kutokana na kata wanazoongoza kuwa na changamoto mbalimbali.
“Ukweli lazima niseme hata kama wao wamepunguza hizi safari lakini bado kiwango cha fedha ni kikubwa, hata kama ni bajeti ya Waziri Mkuu wao kama madiwani wana uwezo wa kukaa na kuamua ziende kwenye kazi fulani na sio safari na ikapitishwa,” alisema.
Mwishoni mwa wiki iliyopita, CHADEMA ilifanya mkutano na kutoa ufafanuzi juu ya taarifa za safari hiyo ambayo ilinukuliwa na baadhi ya vyombo vya habari kuwa ilikuwa ya kifisadi, kitu ambacho CHADEMA ilisema huo ni mpango wa kuwachafua madiwani hao unaofanywa na CCM kwa lengo la kuwagombanisha na wananchi.
Chanzo: Tanzania Daima

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Kilimanjaro Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa