Home » » SITTA: NDANI YA CCM KUNA RUSHWA

SITTA: NDANI YA CCM KUNA RUSHWA




Na Mwandishi wetu,
Moshi.


SIKU chache baada ya Waziri Mkuu Mstaafu Bw. Frederick Sumaye, kuzungumzia swala la rushwa ndani ya chaguzi za Chama Cha Mapinduzi, (CCM), Waziri wa Afrika Mashariki, Bw. Samwel Sitta, amekiri kuwepo hali ya rushwa ndani ya chama hicho na kusema wale wanaosababisha hali hiyo dawa yao iko jikoni.

Bw. Sitta aliyasema hayo mjini Moshi, mkoani Kilimanjaro, wakati akitoa salamu zake katika mkutano mkuu wa uchaguzi wa Umoja wa Vijana wa CCM, (UVCCM), mkoani Kilimanjaro, wakati akitokea kwenye ziara ya kikazi Taveta, nchini Kenya.

“Wana CCM tunasemwa mambo fulani fulani na sisi kama watu wazima na wenye busara na hekima lazima tukiri na tutafute njia ya kujirekebisha”, alisema.

Bw. Sitta alisema kuna watu ndani ya CCM ambao wanafikiria maslahi yao binafsi na kwamba tayari wameunda mtandao wao kwa lengo la kutafuta Urais mwaka 2015 ambapo alisema hawatafika popote.

“Huwezi kutengeneza mtandao wa kifedha ndani ya CCM na ukashinda, chama na wanachama wake hawatakuvumilia; CCM inayo katiba yake na ndiyo itakayotumika kuwadhibiti watu wa namna hii wakati ukifika”, alisema.

Alisema ubaguzi ndani ya CCM unaoendelea sasa ndani ya chaguzi CCM zinazoendelea nchini kote umetokana na wale wanaotumia fedha zao kujitengenezea mitandao ili wajiinue wao binafsi huku wakisahau maslahi ya chama, nchi na wananchi kwa ujumla.

“Kufikia Novemba, mwaka huu, kutatokea mabadiliko makukbwa ndani ya chama na ambayo baadhi yenu mliochaguliwa leo mtashiriki historia hii na baada ya hapo tutazunguka nchi nzima kuwaelezea wananchi hatma ya nchi yetu”, alisema.

Kuhusu vijana Bw. Sitta alitahadharisha ya kuwa ikiwa hawataenziwa kulingana na umuhimu wao kwa kupewa maisha bora CCM na nchi kwa ujumla itayumba.

“Namna ya kuwaenzi vijana ni kuhakikisha wanaishi maisha mazuri na marefu, si unashiba wewe tu huku ukiwaacha wakilala njaa kisha wakichachamaa unasema hawana adabu”, alisema huki akishangiliwa kwa nguvu na vijana hao.

Aidha Waziri Sitta alielezea kusikitishwa kwake na baadhi ya viongozi wa kisiasa haswa wa upinzani wanaotumia changamoto za kimaisha zilizopo kwa kuwadanganya na kuwachanganya wananchi huku wakiwapa matumaini ya kuwapa huduma zikiwemo za bure.

“Kazi ya serikali ni kutafuta njia ya kuwawezesha wananchi ili waondokane na umasikini, wapate mapato, walipe kodi na mwishowe wapate huduma nzuri na si kuwaliwaza ili wabaki na umasikini wao huku ukiwaahidi ya kuwa ukishika madaraka utawapa huduma za bure, hizo ni siasa za kipuuzi na ambazo hazina maana"alisema.
 
Blogzamikoa


0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Kilimanjaro Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa