Home » » Wafanyakazi watekwa, waporwa mil. 220/-

Wafanyakazi watekwa, waporwa mil. 220/-

WATU wanaodhaniwa kuwa majambazi wamewateka wafanyakazi wa Kampuni ya Ujenzi ya DOTT Service Ltd ya nchini Uganda akiwemo mkurugenzi wake wa fedha, Shuresh Bab (45) na kuwapora fedha sh milioni 220.
Majambazi hayo ambayo idadi yake haikufahamika, inadaiwa yalikuwa na ofisa wa polisi na baada ya tukio walifanikiwa kutokomea kusikojulikana huku wakiwatelekeza wafanyakazi hao na gari walilokuwa wakitumia kando ya Mto Karanga mjini Moshi.
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Kilimanjaro, ACP Robert Boaz, alithibitisha kutokea kwa tukio hilo na kwamba tayari hadi sasa watuhumiwa wanne muhimu wa tukio hilo wamekamatwa wakiwa na kiasi cha fedha ambazo zinadaiwa kuporwa.
Boaz alisema tukio hilo lilitokea juzi saa 4:00 asubuhi katika maungio ya barabara ya Arusha na Old Boma ambapo mkurugenzi huyo, Bab, akiwa na watumishi wengine alichukua fedha sh milioni 220 toka katika benki ya Standard Chartered tawi la Moshi.
“Watumishi hao wa Kampuni ya Dott inayojenga barabara ya Same- Mkumbara, walikuja hapa mjini kwa ajili ya kuhamisha fedha kutoka benki ya Standard Chartered ili wazipeleke benki nyingine ya NMB kwa ajili ya kurahisisha malipo ya mshahara wa watumishi wao huko Same,” alisema.
Alisema wakiwa njiani na fedha hizo kuelekea NMB katika gari aina ya Toyota Hilux Double Cabin lenye namba za usajili T 864 AZM, likiendeshwa na Wenslaus Mambo (32), walisimama kupisha pikipiki iliyokuwa inakatisha barabara mbele yao kwenye maungio ya barabara.
Boaz alisema ghafla walijitokeza watu wawili waliokuwa kando ya barabara wakafungua milango ya gari na kuingia ndani na kumwamuru dereva aendeshe kuelekea eneo la Shanty Town na kwamba wakati wakielekea, Bab alifanikiwa kuruka toka garini na kutoa taarifa polisi.
Kwa mujibu wa kamanda, hatua za haraka za ufuatiliaji wa tukio hilo zilifanyika na kufanikiwa kulipata gari hilo likiwa eneo la Mto Karanga pamoja na wafanyakazi hao.
“Mpaka sasa haijafahamika kama kuna silaha yoyote ilitumika katika utekaji huo, huenda ukawa ulikuwa ni mpango, lakini tunaendelea na uchunguzi wa kina ingawaje tunao watu wanne muhimu na majina yao kwa sasa tunayahifadhi kwa ajili ya uchunguzi zaidi na tumefanikiwa kuokoa sh milioni 83,” alisema Boaz.
Alipotakiwa kuthibitisha ushiriki wa ofisa wa polisi katika tukio hilo, Kamanda Boaz hakuweza kukiri ama kukataa akisema ni mapema sana kutaja majina ya wahusika.
Hata hivyo, Boaz alisema njia iliyotumika kusafirisha fedha hizo ni ya kizamani sana na kwamba wahusika walikuwa wana uwezo wa kuzihamisha kwa mawasiliano ya benki na benki.
Chanzo: Tanzania Daima

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Kilimanjaro Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa