Home » » Polisi yadhibiti wafanyabiashara

Polisi yadhibiti wafanyabiashara

MPANGO wa wafanyabiashara wanaosafirisha mazao kwenda Kenya wa kutaka kuzuia magari kutoka Kenya kuingia Tanzania, juzi ulikwama baada Jeshi la Polisi kuimarisha ulinzi katika mpaka wa Holili.
Hatua ya wafanyabiashara hao kutaka kuweka kizuizi mpakani hapo inatokana na mgogoro uliopo sasa baina ya uongozi wa mkoa na wafanyabiashara hao kutokana na kusitishwa kwa ghafla vibali vya kusafirisha mazao hayo kwenda nje ya nchi.
Juzi, saa 1:30 asubuhi  katika eneo hilo la mpakani kulishuhudiwa zaidi ya malori 20 yaliyosheheni mahindi na maharage yakiwa yameegeshwa kando ya barabara ya Holili huku askari zaidi ya saba wakiwa na silaha za moto wakizunguka.
Tanzania Daima ilifanikiwa kuzungumza na mwenyekiti wa mawakala wa mazao hayo, Ramadhan Lema, ambaye alikiri kuwepo kwa mgogoro baina yao na serikali ya mkoa kutokana na hatua yake ya kusitisha ghafla vibali vya kusafirisha mazao hayo kwenda nje ya nchi.
Mbali na kusitisha vibali hivyo pia serikali ya mkoa wa Kilimanjaro imeiteua kampuni ya Kilimanjaro Uchumi (KUC-Ltd ) kuchukua jukumu la usafirishaji wa mazao hatua ambayo inapingwa na wafanyabiashara hao.
Alisema endapo jambo hilo halitamalizwa haraka, watadai haki yao kwa kuweka zuio kwa  kampuni yoyote au mfanyabiashara asiruhusiwe kupita katika mipaka hiyo ya Tanzania na Kenya hadi hapo uamuzi uliotolewa utakapotolewa ufafanuzi wake.
“Hatutafanya vurugu wala kuandamana, isipokuwa tutatumia njia za haki kwa kuweka pingamizi mahakamani ili haki itendeke.Kimsingi suala hili linaweza kumalizwa na Waziri wa Kilimo, Chakula na Ushirika.
“Sisi tumepewa vibali, tunalipa mapato na tunaiingizia nchi yetu fedha za kigeni lakini cha ajabu kampuni ya uchumi ya mkoa imepewa jukumu hilo bila ya kutangazwa zabuni,” alisema Lema.
Alisema kutokana na hatua hiyo ya serikali ya mkoa kuweka zuio la kuuza mazao yao Kenya hadi sasa  zaidi ya tani 8,000 za mahindi na maharage  zimekwama katika mji mdogo wa Himo ukiwemo mchele tani 1,200 huku wafanyabiashara wa Kenya waliokuwa wakishirikiana na Watanzania wakitaka kuondoa mitaji yao waliyowekeza.
Mkuu wa Mkoa wa Kilimanjaro, Leonidas Gama, alisema serikali haijasitisha biashara hiyo kama inavyodaiwa na baadhi ya wafanyabiashara hao wa nafaka huku akiwataka wafanyabiashara hao kuendelea na bishara yao kama kawaida.
Naibu Waziri wa Chakula, Kilimo na Ushirika, Adam Malima, alipotakiwa kutolea ufafanuzi sakata hilo, alisema uamuzi huo umetolewa na serikali ya mkoa ambayo imelenga kukusanya mapato na kuongeza nguvu ya kiuchumi kwa kuhimiza matumizi ya soko la kimataifa la nafaka lililo katika mji mdogo wa Himo, Wilaya ya Moshi.
Chanzo;Tanzani Daima

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Kilimanjaro Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa