Home » » Wanne wanaswa ujambazi Kilimanjaro

Wanne wanaswa ujambazi Kilimanjaro

JESHI la Polisi mkoani Kilimanjaro linawashikilia watu wanne wanaodaiwa kuwa majambazi kwa kushiriki katika matukio ya unyang’anyi na uporaji yaliyotokea hivi karibuni katika maeneo mbalimbali mkoani hapa.
Kaimu Kamanda wa Polisi mkoani hapa, Koika Moita, aliwaambia waandishi wa habari jana kuwa Desemba 17, majira ya saa nane mchana katika Kata ya Kiusa Mjini, Moshi, jeshi hilo lilifanikiwa kuwatia watuhumiwa hao mbaroni ambao hata hivyo hakuwataja majina kwa madai kwamba upelelezi unaendelea.
Moita alisema kuwa jeshi hilo limefanikiwa kuwakamata watuhumiwa hao baada ya kufanya msako mkali kutokana na kuongezeka kwa matukio ya uporaji na unyang’anyi kwenye maduka makubwa, vituo vya mafuta pamoja na makazi ya watu.
Jeshi hilo lilifanikiwa kumkamata dereva wa gari aina ya Mark II yenye namba T 564 AUW aliyetambulika kwa jina la Nickson Urio lililokuwa likitumiwa na wahalifu hao wa ujambazi.
“Watu hao wamekuwa wakijihusisha na ujambazi katika maeneo mbalimbali, na sasa walikuwa wanajiandaa kufanya uhalifu sehemu mbalimbali za mkoa huu, hivyo polisi tupo makini na tunawahakikishia wananchi usalama, na tutaendelea kuwakamata wote wanaojihusisha na vitendo hivi,” alisema Moita.
Aliongeza kuwa watuhumiwa walikiri kushiriki katika matukio mbalimbali ya uporaji, na walipopekuliwa walikutwa na bunduki aina ya short-gun ambayo imekatwa mtutu na kitako chake huku ikiwa haina namba.
Walikutwa pia na vitu mbalimbali, zikiwemo kompyuta mpakato mbili, vibao vya namba za magari vitatu, funguo za magari, simu nane pamoja na vocha za mitandao mbalimbali ya simu ambazo hazijajulikana thamani yake.
Chanzo;Tanzania Daima

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Kilimanjaro Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa