Home » » CHADEMA: Fedha za maendeleo haziwafikii wananchi

CHADEMA: Fedha za maendeleo haziwafikii wananchi

CHAMA cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) kimedai kuwa fedha zinazoidhinishwa na Bunge la Bajeti la Jamhuri ya Muungano kwa ajili ya matumizi ya kawaida na shughuli za maendeleo ya wananchi haziwafikii wananchi ipasavyo kwa baadhi ya halmashauri, ikiwemo ya Manispaa ya Moshi kwa mwaka wa fedha wa 2013/14.
Hayo yalibainishwa na Mkurugenzi wa Sheria wa CHADEMA, Tundu Lissu, wakati wa mikutano ya Operesheni M4C Pamoja Daima katika mikoa ya Kanda ya Kaskazini inayoendelea akisaidiana na Mwenyekiti wa Baraza la Vijana la CHADEMA (BAVICHA) Taifa, John Heche.
“Nataka niulize fedha zetu tulizotenga bungeni kwa ajili ya Halmashauri ya Moshi ziko wapi? Kila mwaka tunatenga bajeti kwa kila halmashauri na kila mkoa na zikishatengwa zinatakiwa zipelekwe kunakohusika na zitumike kama zilivyoelekezwa,” alisema Lissu.
Alitolea mfano bajeti iliyotengwa kwa mwaka huu wa fedha kwa matumizi ya kawaida katika Mkoa wa Kilimanjaro ni sh bilioni 175 huku sh bilioni 32.7 zikitengwa kwa ajili ya maendeleo katika mkoa.
Lissu alisema sh bilioni 135 zilitengwa kama ruzuku ya mishahara na kati ya fedha hizo, Manispaa ya Moshi ilitengewa sh bilioni 16 huku mkoa ukitengewa kiasi cha sh bilioni 17 kwa ajili ya matumizi mengineyo na Manispaa ya Moshi ikitengewa sh bilioni 2.4.
Alisema kwa mujibu wa kitabu cha orodha ya majedwali yanayoambatana na hotuba ya waziri mkuu, kuhusu makadirio ya matumizi ya  fedha cha mwaka 2013/2014, Mkoa wa Kilimanjaro umetengewa sh bilioni 14 kwa ajili ya mfuko wa barabara huku halmashauri ya Manispaa ya Moshi ikitengewa sh bilioni 3.
“Mafungu yote haya ukiwauliza madiwani zimekuja? Watakwambia hatujaziona, kama madiwani hawajaziona zimekwenda wapi? Haya mabilioni yanayozungumzwa kwenye hiki kitabu yamekwenda wapi? Kama ni hewa kwanini wameyaandika, kwanini wasiseme ukweli?” alihoji Lissu.
Alisema ni vema serikali ikasema ukweli kwamba fedha hakuna kuliko kudanganya kwa kuweka kiasi kikubwa cha fedha katika vitabu hali inayowatia shaka wananchi ya kuwa kama fedha hizo hazikufika basi huishia mikononi mwa mafisadi.
“Ni bora viongozi watuambie kwamba hatuna hela, kwanini wanaweka mabilioni makubwa haya? Wanataka wamdanganye nani? Na kama ni mabilioni makubwa namna hii wanaleta chache, tutajuaje kama hazijaibiwa? Tutajuaje kama hizo ambazo hazikuja, hazikuja kwa sababu ya ufisadi?” alihoji Lissu.
Alisema tabia hiyo imekuwa ikifanyika kila mwaka na kwamba ili kuondokana na hali hiyo, ni vema wananchi wakaamua kuchagua CHADEMA wakati wa uchaguzi, ili waweze kuona matunda ya nchi yao.
“Uchaguzi wa kata moja ya Tanzania si mdogo, kwa sababu ili tuwashinde CCM kwenye chaguzi kubwa lazima tuwashinde kuanzia chini, tuwashinde kwenye vitongoji, tuwashinde kwenye mitaa, tuwashinde kwenye kata, tuwashinde kwenye majimbo na tuwashinde kwenye urais, ndiyo nchi itakuwa salama, na wakati umefika wa kufanya hiyo kazi, tusipoifanya CCM watatuangamiza,” alisema Lissu.
Mwenyekiti wa BAVICHA Taifa, Heche, aliitahadharisha CCM kuacha kutoa rushwa ya mahindi kwa ajili ya chakula yanayodaiwa kupelekwa katika Kata ya Kiboriloni kwa lengo la kuwagawia wananchi ili wawapigie kura katika uchaguzi mdogo wa udiwani utakaofanyika hivi karibuni.
Heche aliitaka Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa nchini (TAKUKURU) kufuatilia juu ya madai ya kuwepo kwa fedha kiasi cha sh milioni 5.5 zilizotengwa kwa ajili ya kununulia mahindi na kisha kuyagawa kwa wakazi wa Kata ya Kiboriloni
Chanzo;Tanzania Daima

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Kilimanjaro Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa