Home » » MANISPAA MOSHI KUWACHUNGUZA VIJANA

MANISPAA MOSHI KUWACHUNGUZA VIJANA

Moshi.Halmashauri ya Manispaa ya Moshi inachunguza mwenendo wa vijana wanaokamata magari yanayodaiwa kuegeshwa vibaya kutokana na malalamiko makubwa kuwa zoezi hilo linatawaliwa na ubabe.
Meya wa Manispaa hiyo, Jaffar Michael alisema endapo vijana hao watashindwa kutumia busara na sheria zilizopo, halmashauri haitasita kuchukua uamuzi mgumu wa kuwaondoa kazini.
Malalamiko makubwa ni baadhi ya vijana hao kujihusisha na vitendo vya rushwa, kuingia kwa nguvu kwenye magari yanayodaiwa kuegeshwa vibaya na kutanguliza zaidi faini badala ya kuzuia makosa.
Baadhi yao wamejikuta wakiambulia kipigo kutoka kwa wamiliki wa magari pale wanapojaribu kumnyang’anya dereva funguo na vipigo hivyo vimekuwa vikiungwa mkono na wananchi wengine.
“Suala la uegeshaji mbaya linanisumbua sana, malalamiko ni mengi. Shida ni kwamba, hata ukileta wakala mwingine anawatumia vijana walewale wanaolalamikiwa,” alisema Meya.
Meya alisema ingawa sheria ndogo inayosimamia makosa hayo inataka faini iwe ni Sh50,000, lakini baadhi ya vijana hao hutoza faini ya hadi Sh100,000 kwa wamiliki wa magari ambao ni wageni.
Mmoja wa wamiliki wa magari, Adelina Shayo maarufu kama Mama Changbay, alilalamikia kutozwa Sh20,000 eneo la Benki ya NMB Tawi la Nelson Mandela wakati alikuwa bado hajaegesha gari hilo.
“Nimeshuka tu kwenye gari ili niangalie kama nimeegesha vizuri ama la ghafla wakaingia vijana kwenye gari yangu wananiambia nimeegesha vibaya gari…nchi haiwezi kuendeshwa kwa staili hii,” alilalamika.
Mfanyabiashara huyo aliyekuwa na gari aina ya Toyota Spacio namba T103 CCQ alilipishwa faini ya Sh20,000 badala ya Sh50,000 na kupewa stakabadhi ya halmashauri namba 247724 ya Januari 3.
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Kilimanjaro, Robert Boaz alisema ofisi yake inafahamu kuwapo kwa kero hiyo, lakini akasema tatizo ni kugeuza faini kuwa ndiyo chanzo cha mapato ya halmashauri.
Chanzo:Mwananchi

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Kilimanjaro Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa