Home » » NDESAMBURO ALIA NA MABARAZA KUKOSA NGUVU

NDESAMBURO ALIA NA MABARAZA KUKOSA NGUVU

MBUNGE wa Moshi Mjini, Philemon Ndesamburo, (CHADEMA) amesema mabaraza ya manispaa kushindwa kuwawajibisha watendaji wazembe kimekuwa chanzo cha kuendelea kuwepo kwa ufisadi kwenye halmashauri nyingi nchini.
Ndesamburo aliyasema hayo juzi katika kikao cha baraza la madiwani kilichokuwa kikijadili bajeti ya mwaka 2014/15, ambapo wajumbe wa kikao hicho walilalamikia idara ya manunuzi inayodaiwa kushamiri kwa rushwa.
Alisema kuwa wakurugenzi wengi wamekuwa chanzo cha watendaji kuendelea kufanya vibaya, huku wakipuuza maazimio yanayofanywa na wawakilishi wa wananchi na kushindwa kuwaletea wananchi maendeleo.
“Wakurugenzi wengi wanapofanya vibaya unakuta mabaraza ya madiwani yanaishia kuazimia kuwafungia nje au kususia vikao lakini ukweli ni kwamba bado wanakuwa hawajamaliza tatizo,” alisema.
Alisema kuwa kutokana na madiwani kuwa viongozi wa mabaraza wanapaswa kuwa na mamlaka ya kuwawajibisha watendaji wababaishaji wakiwemo wakurugenzi.
Ndesamburo hakusita kumzungumzia Mkurugenzi aliyemaliza muda wake, Bernadette Kinabo, kuwa alikuwa mzigo, kwa kuwa alishindwa kusimamia maazimio mengi yaliyofanywa na madiwani kwenye vikao, hivyo kushindwa kutekelezwa.
Hata hivyo kauli hiyo ilipingwa na Mkurugenzi mpya wa manispaa hiyo, Shaaban Ntarambe, ambaye alimtetea mkurugenzi huyo.
Ntarambe alisema kuwa hakuna tofauti zozote ambazo yeye ameona zilizokuwepo kwa mkurugenzi huyo bali alikuwa akifuata taratibu za kisheria.
Aidha, kikao hicho kilipitisha bajeti ya sh bilioni 47.8 kwa ajili ya utekelezaji wa shughuli mbalimbali za  maendeleo kwa mwaka 2014/2015.
Chanzo;Tanzania Daima

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Kilimanjaro Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa