MWENYEKITI
wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ardhi, Maliasili na Mazingira, James
Lembeli, amesema kuwa kiasi cha fedha zilizotengwa kwa ajili ya
Operesheni Tokomeza Ujangili hazijulikani zilipo.
Alisema kuwa hatua hiyo imesababisha askari zaidi ya 2,000 waliounda
kikosi maalumu kwa ajili ya operesheni hiyo ambayo imesitishwa kwa muda
kuanza kudai posho zao.
Lembeli aliyasema hayo mwishoni mwa wiki wakati kamati hiyo
ilipotembelea Hifadhi ya Taifa ya Mlima Kilimanjaro (Kinapa) kwa ajili
ya kujionea namna hifadhi hiyo ilivyofanikiwa kudhibiti uharibifu wa
mazingira na kutunza bioanuai ya eneo la ukanda wa hifadhi ya nusu
maili.
Alisema kuwa hadi sasa kiasi cha sh bilioni 1.5 za posho hizo hakijalipwa kwa askari hao.
Lembeli alisema katika operesheni hiyo iliyoanza mwanzoni mwa mwaka
2013 na baadaye kusitishwa Novemba mosi, serikali ilikuwa imetenga zaidi
ya sh bilioni 3.5, lakini inashangaza kuambiwa kuwa askari bado wanadai
posho zao.
Alisema baada ya operesheni hiyo kusitishwa kutokana na ripoti ya
kamati yake iliyotolewa mwishoni mwa mwaka jana bungeni, askari hao bado
walikuwa wakiendelea na kazi huku wakisubiri kuanza kwa awamu ya pili
ya operesheni hiyo.
“Serikali ilitenga zaidi ya sh bilioni 3.5 zitumike katika Operesheni
Tokomeza, inashangaza sana kuambiwa kuwa askari wale wanaendelea
kusotea posho zao hadi sasa,” alisema.
Kwa mujibu wa Lembeli, kusitishwa kwa operesheni hakukumaanisha
kwamba ndiyo ukomo wake, kwani askari waliendelea kulinda usalama wa
maeneo yale, na kwamba katika kazi hiyo ambayo wameifanya kwa moyo mmoja
hadi sasa, walitakiwa kulipwa stahili zao.
Askari walioshiriki operesheni hiyo ni wanajeshi 480 kutoka Jeshi la
Wananchi wa Tanzania (JWTZ), polisi 440, wamo pia askari 440 kutoka
Kikosi dhidi ya Ujangili (KDU), askari wa wanyamapori kutoka Shirika la
Hifadhi za Taifa (Tanapa) na Usalama wa Taifa.
Wengine ni askari 99 kutoka Wakala wa Huduma za Misitu (TFS) na
askari wanyamapori 51 kutoka Mamlaka ya Hifadhi ya Ngorongoro (NCAA).
Alisema ili kuondoa sintofahamu hiyo, kamati inashauri kufanyika kwa
ukaguzi wa fedha hizo pamoja na serikali kutoa ufafanuzi wa kiasi
kilichobaki kwa kueleza sababu za ucheleweshaji wa malipo ya askari hao
wakati bajeti hiyo tayari ilikwishapitishwa.
Wakati huo huo, kamati hiyo imekutana na kushauriana na Menejimenti
ya Hifadhi za Taifa (Tanapa) na Hifadhi ya Taifa ya Mlima Kilimanjaro
(Kinapa) kuhusu viwango vya tozo za utalii kwenye mlima huo.
Waliitaka serikali kulipa fursa shirika hilo kupanga viwango vya tozo
za viingilio vya utalii nchini ili kuvifanya viendane na hali halisi ya
utalii duniani badala ya utaratibu wa sasa ambao hauipi nafasi Tanapa
kupanga viwango hivyo.
“Haya mambo tatizo hapa ni siasa, serikali inatakiwa kuangalia tozo
zake na kuacha hadithi ya kunufaisha wafanyabiashara ambao hata hivyo
hawalipi kodi.
“Hifadhi ikipewa mamlaka kamili ya kujiendesha lazima nchi ipate
faida, lakini kwa staili hii tusipowatetea hawa Tanapa, shirika hili
litakufa kama lilivyokufa Shirika la Ndege nchini (ATCL),” alisema.
Ushauri wa Kamati ya Lembeli, unafananishwa na taarifa za serikali
ambazo zinaonyesha kwamba kwa sasa mlima Kilimanjaro unaonekana kuzidiwa
na idadi ya watalii.
Takwimu zinaonyesha kuwa katika kipindi cha miaka mitano iliyopita,
mlima Kilimanjaro kwa mwaka ulikuwa ukipokea wageni 13,000, lakini hivi
sasa watalii wanaopanda mlima huo ni zaidi ya 50,000 huku wapagazi
wakidaiwa kuwa zaidi ya 200,000 kwa mwaka.
Akizungumzia changamoto hiyo, Mkurugenzi Mkuu wa Tanapa, Allan
Kijazi, alisema shirika hilo limeweka mikakati ya kuona njia mbadala ya
kupunguza idadi ya watu wanaopanda mlima ambapo tayari wameshaanza
kuwasiliana na vyama vya wafanyabiashara ya uongozaji wa utalii kuhusu
mpango huo.
Kuhusu eneo la hifadhi ya nusu maili, Kijazi alisema Tanapa imeandaa
mpango utakaohakikisha ukanda huo unasimamiwa na kupunguza uharibifu wa
mazingira kikamilifu ambapo rasimu ya muongozo huo imeshaandikwa.
Chanzo;Tanzania Daima
0 comments:
Post a Comment