Home » » POLISI KILIMANJARO YAMSAKA PAPAA

POLISI KILIMANJARO YAMSAKA PAPAA

Kamanda wa Polisi Mkoa wa Kilimanjaro, Robert BoazJESHI la Polisi mkoani Kilimanjaro, limeungana na Idara ya Uhamiaji kumsaka mfanyabiashara Emmanuel Kisima maarufu kwa jina la ‘Papaa’ anayetuhumiwa kuwa kinara wa mtandao wa kusafirisha wahamiaji haramu.

Mfanyabiashara huyo kwa sasa yupo mafichoni katika moja ya majiji hapa nchini akijaribu kukwepa mkono wa dola huku watu wa karibu naye wakijaribu kuficha ukweli wakidai yuko nje ya nchi, lengo likiwa ni kuvihadaa vyombo vya dola visibaini mahali alipo.
Akizungumza na Tanzania Daima mwishoni mwa wiki, Kamanda wa Polisi Mkoa wa Kilimanjaro, Robert Boaz, alisema tayari jeshi hilo limeanza mchakato wa kumsaka mfanyabiashara huyo ambaye amekuwa akitumia jina la Mkuu wa Jeshi la Polisi nchini mstaafu (IGP), Said Mwema kutekeleza uhalifu wake.
Kamanda Boaz ametoa wito kwa wananchi wenye taarifa sahihi za mahali alipo mfanyabiashara huyo kwenda kutoa taarifa huku Idara ya Uhamiaji nayo ikitoa rai kwa raia wema kumfichua.
Papaa anatuhumiwa kusafrisha kundi la wahamiaji haramu 56 kutoka Ethiopia ambao walikamatwa Desemba 7 mwaka jana wakiwa ndani ya gari T 188 AYU Fuso katika Kijiji cha Jiungeni, Kata ya Ruvu, Wilaya ya Same.
Baada ya kukamatwa kwa wahamiaji hao haramu akiwamo dereva wa gari hilo, mfanyabiashara huyo alijaribu bila mafanikio kutaka kuwahonga maofisa wa polisi, ili waliachilie gari hilo, lakini juhudi hizo ziligonga mwamba na ndipo alipoamua kukimbilia mafichoni.
Hivi karibuni, IGP Ernest Mangu, aliagiza Jeshi la Polisi mkoani Kilimanjaro kumsaka na  kumtia mbaroni mfanyabiashara huyo kutokaana na kutumia vibaya jina la mtangulizi wake, Said Mwema.
Chanzo;Tanzania Daima
Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399.

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Kilimanjaro Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa