Home » » Shahidi aeleza mengi mauaji ya polisi Mwanga

Shahidi aeleza mengi mauaji ya polisi Mwanga

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 
Kamishna Msaidizi (ACP) Duan Nyanda ameieleza mahakama kuwa mshtakiwa Samwel Saitoti alimpiga risasi ya kichwa Konstebo Michael Milanzi na kufumua ubongo wake.
Nyanda, ambaye pia ni Mkuu wa Upelelezi wa Makosa ya Jinai (RCO) Mkoa wa Arusha ndiye aliyeandika maelezo ya onyo (caution statement) ya mshtakiwa huyo ambaye ni raia wa Kenya.
“Aliniambia yeye (Saitoti) ndiye alimpiga PC Milanzi risasi ya kichwa ikafumua ubongo na wenzake walikuwa na kazi ya kumdhibiti yule polisi mwingine aliyekuwa lindo na marehemu,” alisema.
Siku ya mauaji hayo Julai 11,2007 yaliyoambatana na uporaji wa Sh.239 milioni mali ya Benki ya NMB Tawi la Mwanga, Milanzi alikuwa lindoni na polisi mwenzake, PC. Naftal Asher Magoma.
Akitoa ushahidi wake mbele ya Jaji Kakusulo Sambo, Ijumaa iliyopita ACP Nyanda alisema Saitoti alimweleza kuwa baada ya kumuua, alimwamuru PC Magoma kulala juu ya mwili wa mwenzake.
“Wakati namuhoji aliniambia biashara ya kwenda kupora benki ilishirikisha Watanzania na kwamba baada ya mipango kukamilika walitumia magari ya wizi kwenda kupora na kufanya mauaji,”alisema.
Akiongozwa na Wakili wa Serikali,Stella Majaliwa kutoa ushahidi wake, Nyanda alisema mshtakiwa huyo alimweleza kuwa, baada ya mauaji hayo yeye alichukua bunduki Ya marehemu aina ya SMG.
Hata hivyo Jaji Sambo alikataa kupokea maelezo ya mshtakiwa huyo ili yawe kielelezo katika kesi hiyo inayovuta hisia za wengi, kutokana na kubainika yalichukuliwa nje ya muda ulioruhusiwa kisheria.
Jaji Sambo alisema, sheria inataka maelezo ya mtuhumiwa yachukuliwe si zaidi ya saa nne tangu kukamatwa kwake na endapo muda huo utapita, ofisa wa Polisi ataongeza muda wa saa nane.
Alisema katika kesi hiyo, mshtakiwa alikamatwa Julai 20,2007 na kusafirishwa hadi Moshi siku hiyo hiyo lakini maelezo yake yakachukuliwa saa 4:00 asubuhi ya Julai 22 ikiwa ni siku mbili baadaye.
Wakati huo huo, Shahidi wa 10, Mrakibu wa Polisi (SP) Zakaria Benard alidai, Saitoti na mshtakiwa wa pili, Peter Kimani pia ni raia wa Kenya walitambuliwa katika gwaride la utambulisho.
Akitoa ushahidi wake kwa kuongozwa na wakili wa Serikali, Ladslaus Komanya, shahidi huyo alidai kati ya mashahidi 10 walioitwa katika gwaride hilo lililofanyika Agosti 1,2007, mashahidi tisa waliwatambua washtakiwa hao.
Chanzo;Mwananchi

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Kilimanjaro Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa