Home » » Wanakijiji wafunga Barabara ya Kia

Wanakijiji wafunga Barabara ya Kia

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 

  Wakazi wa vijiji vinne vinavyopakana na Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Kilimanjaro (Kia), jana mchana walifunga kwa muda barabara ya kutoka nje ya uwanja huo na kuzuia hali ya sintofahamu kwa wageni.
Wananchi hao wanapinga kile wanachodai ni mpango wa Serikali kuwapora ardhi ya vijiji vyao kwa madai kuwa baadhi yao wamevamia kwenye maeneo yanayomilikiwa kihalali na Kia.
Hata hivyo, Polisi wa Kutuliza Ghasia (FFU) walifanikiwa kuwashawishi wananchi hao, wengi wao wakiwa wanawake wa kabila la Wamasai, kufungua barabara hiyo na kukusanyika pembezoni mwa barabara.
Tukio hilo lilitokea saa 9:00 mchana baada ya wananchi hao kushindwa kuafikiana katika kikao kilichoshirikisha wanavijiji wa Sanya Stesheni, Tindigani, Mtakuja na Majengo.
Kamanda wa Polisi Mkoa Kilimanjaro, Robert Boaz jana alilithibitishia gazeti hili kuhusu wananchi hao kufunga barabara kwa muda, lakini akasema polisi waliokwenda eneo hilo wamedhibiti hali hiyo.
“Ni kweli kuna wananchi walifunga barabara, lakini tumezungumza nao na wameifungua kwa hiyo hali sasa ni shwari na magari yanapita kama kawaida,” alisema Boaz.
Boaz alisema KIA ilipimwa mwaka 1989, lakini wakati huo tayari kulikuwa na vijiji vilivyoandikishwa na baadhi ya wananchi waliingia hadi eneo la uwanja huo.
“Kumekuwa na jitihada za viongozi kutatua mgogoro huu na wiki mbili zilizopita Mkuu wa Mkoa (Leonidas Gama) na kamati nzima ya ulinzi na usalama tulikwenda kuzungumza nao,” alisema.
Kwa mujibu wa Kamanda Boaz, katika kikao hicho hawakufikia muafaka na ndipo baadhi yao walipohamasishana kwenda kufunga barabara ya kwenda KIA hadi polisi walipowaondoa.
Chanzo;Mwananchi

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Kilimanjaro Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa