Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399.
Mwanafunzi wa shule ya msingi Ghona akionyesha choo cha shule ya jirani wanachokitumia, ambacho nacho pia kimejaa.
Kilimanjaro ya zamani sio ya sasa. Ile sifa ya mkoa huo kinara wa elimu nchini ilishaporomoka siku nyingi.
Zamani ilikuwa ni jambo la ajabu kusikia kuwa kuna
shule katika mkoa huo ikikabiliwa na changamoto zinazoepukika kama vile
ukosefu wa madawati, vyumba vya madarasa, matundu ya vyoo na walimu.
Hata hivyo, Kilimanjaro ya leo hasa wilaya maarufu
ya Moshi ina shule ambazo wasimamizi wake wameshindwa kujenga hata
miundombinu ya vyoo.
Angalau basi ingekuwa shule moja, la hasha! Ni
shule kadhaa ambazo kwa hali ilivyokuwa tete, wanafunzi na walimu
wanalazimika kujisitiri porini au katika nyumba za jirani na shule zao.
Wakati tatizo la ukosefu wa matundu ya vyoo
likishtadi hasa katika shule za msingi za Ghona, Makame juu, Mabirang’a
na Sagana, viongozi, wazazi na jamii kwa jumla wanarushiana mpira kuhusu
ufumbuzi wa kadhia hiyo inayoitia doa wilaya ya Moshi.
Hali halisi
Shule ya Msingi Saghana iliyoanza mwaka 2005
haijawahi kuwa na choo kabisa hali inayowalazimu walimu pamoja na
wanafunzi kujisasaidia vichakani au katika vyoo vya nyumba zilizopo
jirani na shule.
Mwenyekiti wa kamati ya shule hiyo, Haruni Msuya,
anakiri kuwa hiyo ni fedheha kwa walimu na wanafunzi, lakini anaitupia
mzigo serikali kwa kukubali kuisajili shule hiyo ikiwa haina choo.
“Mwandishi hata sisi hatufurahi shule yetu
kutokuwa na choo. Ni aibu kwetu lakini kama unavyoona wazazi walichangia
shule ikajengwa na sasa hali ya maisha imekuwa ngumu ukimwambia mzazi
achangie kunakuwa na mvutano,’’ anasema.
Anasema kinachokwaza maendeleo shuleni hapo
ikiwamo ujenzi wa choo, ni baadhi ya wanasiasa kuingilia miradi ya
maendeleo wakiwaeleza wananchi kuwa ujenzi ni jukumu la serikali.
“Hapa tunajitahidi kuwaelimisha wazazi kuhusu
umuhimu wa kuchangia elimu, lakini wanasiasa nao wanapita wakiwaambia
wazazi msichangie… inakuwa nivute nikuvute na ndio maana elimu hapa
haiendelei anaeleza Msuya.
Kwa upande wake, Diwani wa kata ya Makuyuni ilipo
shule hiyo, Mangachi Mrema anasema jitihada za ujenzi za wa choo kipya
zinafanyika na sasa wameanza na uchimbaji wa shimo.
Katika Shule ya Msingi Ghona, wanafunzi wanalazimika kujisaidia
vichakani huku wengine wakijisaidia katika shule jirani ya Mabiranga
ambayo nayo haina matundu ya kutosha. Shule hiyo ina matundu nane tu
yanayotumiwa na wanafunzi 720 wakiwamo wa shule jirani ya Ghona.
Kwa mujibu wa taratibu za kielimu kama
zinavyoainishwa na Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi, tundu moja la
choo linapaswa kutumiwa na wanafunzi 25 ambao ni wa kiume. Kwa
wanafunzi wa kike tundu moja linatumiwa na wanafunzi 20.
Kwa takwimu hizi, ni dhahiri kuwa hivi sasa katika
shule ya msingi Mabiranga inayowasitiri pia wanafunzi wa shule jirani,
tundu moja la choo linatumiwa na wanafunzi 90 kiwango ambacho ni zaidi
ya mara tatu ya utaratibu wa wizara.
Mwenyekiti wa kamati ya shule ya Ghona, Seph
Ngate, anasema shule hiyo haina choo tangu mwaka 2010, kufuatia choo
kilichokuwepo kusombwa na mafuriko.
Anaeleza kuwa pamoja na wazazi kuchangia ujenzi
mpya wa choo, haukukamilika baada ya choo kuporomoka kwa sababu ya
kujengwa chini ya kiwango.
“ Kitendo cha choo kuporomoka kabla ya kukamilika
kimewakatisha tamaa wazazi na kukataa kuendelea kuchangia ujenzi wa
choo na hivyo kusababisha wanafunzi kujisaidia vichakani na wengine
katika shule jirani,’’ anasema.
Diwani wa kata ya Kahe Mashariki, Idd Mchomvu,
anakiri shule ya Ghona kutumia choo kimoja na shule ya mabirang’a lakini
akasema changamoto kubwa ni wazazi kutokuwa na mwamko wa kuchangia.
Anasema hali duni ya maisha inayowakabili wananchi wa kata hiyo imesababisha michango kutochangwa kwa wakati.
Mchomvu anasema tayari wameanza mchakato wa ujenzi
wa choo ili kuwanusuru wanafunzi na magonjwa ya mlipuko. Anasema tayari
wameshapewa Sh 1 milioni kama hamasa ya haramabee ya ujenzi huo.
Shule nyingine ni Makame juu ambayo wanafunzi wanalazimika kujisaidia kwenye mashamba ya migomba kufuatia choo chao kujaa
Serikali inasemaje?
Ofisa Elimu wilaya ya Moshi, Simon Sheshe,
anakiri shule nyingi kukabiliwa na changamoto mbalimbali ikiwemo uhaba
wa madawati, vyoo na miundombinu ya madarasa pamoja na walimu.
Anasema fedha zinazotengwa na serikali kwenye sekta ya elimu ni kidogo hivyo hazitoshi kugawanywa katika kila shule.
Ukiondoa kutumia kiasi kidogo wanachotumiwa na
serikali, ofisa huyo anawashukia wazazi kwa kuwa na mwamko mdogo wa
kuchangia miradi ya elimu wakiamini hilo ni jukumu la serikali.
“Watu huku hawana mwamko wa kuchangia elimu,
wanasubiri kufanyiwa kila jambo hata ukiwahamasisha wachangie hawako
tayari. Wao wanaamini hiyo ni kazi ya serikali tu,” anabainisha
Chanzo:Mwananchi
0 comments:
Post a Comment