Home » » MALALAMIKO: WAFUGAJI WAKENYA WAVAMIA ROMBO

MALALAMIKO: WAFUGAJI WAKENYA WAVAMIA ROMBO

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 
 
Wafugaji wa jamii ya Kimasai kutoka Kenya, wamevamia makazi ya wakulima wilayani hapa na kuingiza mifugo yao kwenye mashamba hali inayosababisha uharibifu wa mazao.
Mbunge wa Jimbo la Rombo, Mkoa wa Kilimanjaro, Joseph Selasini alisema jana kuwa alipofanya ziara ya kushtukiza katika vijiji vya Mwekiyo na Ngareni alikuta makundi zaidi ya 20 ya ng’ombe na mbuzi yakiwa katika mashamba ya wakulima.
Selasini alisema hali hiyo ni hatari kwa usalama wa nchi kutokana na idadi kubwa ya wafugaji kutoka Kenya kuingia nchini kinyume na taratibu za uhamiaji.
Kutokana na hali hiyo, aliitaka Serikali wilayani hapa kufanya kikao cha ujirani mwema na Kenya ili kufanya uamuzi wa kudhibiti uingizwaji wa mifugo hiyo.
 “Wafugaji wa Kenya wanaingiza mifugo katika mashamba ya wakulima wilayani Rombo hasa maeneo ya tambarare hali inayosababisha ukanda huo kukumbwa na baa la njaa kila mwaka,” alisema Selasini.
Alisema hali hiyo isipodhibitiwa mapema, inaweza kusababisha migogoro ya ardhi kati ya Kenya na Tanzania.
Mkulima wa Kijiji cha Mwekiyo, James Lyakurwa alisema wamekuwa wakipeleka malalamiko ya uingizwaji huo holela wa mifugo katika mashamba yao kwa uongozi wa kijiji  lakini hakuna kinachofanyika.
Naye mfugaji Jonathan Waivera kutoka Kenya alipoulizwa sababu za kuingiza mifugo yao hapa nchini, alisema  wameuziwa maeneo hayo ya kulisha mifugo.
Kwa upande wake Mkuu wa Wilaya hiyo, Elinas Palangyo alikiri kuwapo kwa wahamiaji hao na kwamba tayari Serikali imeshavunja mikataba ya mauziano ya mashamba hayo.
 Chanzo:Mwananchi

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Kilimanjaro Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa