Home » » WADAU: BIASHARA YA SANAA BADO WIZI MTUPU

WADAU: BIASHARA YA SANAA BADO WIZI MTUPU

Licha ya Wizara ya Habari, Vijana, Utamaduni na Michezo kuahidi kuwasaidia wasani katika kudhibiti wizi wa kazi zao, wadau wa sanaa nchini wamesema kuwa hawaridhishwi na adhabu zinazochukuliwa na vyombo vyenye mamlaka ya kulinda na kutetea haki za wasanii nchini.
Kutokana na kukithiri kwa wizi na uchakachuaji wa kazi za wasanii, wadau hao wameitaka Serikali kuingilia kati kwa kuwachukulia hatua zinazostahili kisheria wale wote watakaobainika kuhujumu wasanii.
Mbali na kutoridhishwa na hatua zinazochukuliwa pia wamewataka wasanii kufanya kazi zao kwa weledi na ubunifu kwa kuingia darasani na kuacha tabia ya kulipua kwa lengo la kufanya biashara.
“Sanaa ni kazi kama kazi nyingine, kazi ya msanii inahitajika kuheshimiwa na kulindwa kwa mujibu wa sheria, kanuni na taratibu zake na kwa wale wote watakaobainika kuwa wanaihujumu wadhibitiwe na kuwajibishwa,” anasema Edwin Semzaba.
Semzaba ni Mhadhiri kutoka Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM), alieleza hayo wakati alipokuwa akitoa mafunzo kwa vijana toka vikundi vitatu vya sanaa ya maigizo vya Malezi Youth Theatre, Lumumba na Parapanda.
Anasema kwa hapa nchini bado mchango wa taaluma katika sanaa ya maonyesho siyo nzuri, hasa ikizingatiwa kuwa watu wengi wanaamini kuwa ni kipaji hata bila ya kuwa na elimu kitu ambacho siyo kweli.
“Kuna tofauti kubwa kati ya mtu mwenye kipaji na mtu aliyepata mafunzo, kwa kuwa aliyepata mafunzo ana wigo mpana wa kufanya shughuli zake tena kwa ubora kuliko yule mwenye kipaji lakini hana mafunzo,” alibainisha Semzaba.
Semzaba ambaye ni mwandishi wa vitabu, mwigizaji wa Sanaa za Maigizo na Mwenyekiti wa Chama cha Waandishi Vitabu nchini (Uwavita) anasema sanaa ya maigizo ni ngumu na yenye gharama, ikilinganishwa na sanaa za filamu licha ya kuwa inafanya vizuri.
Alisisitiza kuwa iwapo Serikali ingeweka sera madhubuti ambayo itasaidia kulinda na kudhibiti wizi na uchakachuaji wa kazi za wasanii nchini ingeweza kuwainua wao kiuchumi pamoja na pato la taifa kama ilivyo kwenye nchi za wenzetu.
Lakini kutokana na kuwapo kwa ukosefu wa sera hiyo madhubuti wasanii wamekuwa wakilia na kuingia hasara kutokana na kazi zao kuibwa na kuchakachuliwa kila kukicha.
Semzaba ambaye ni mtunzi wa kitabu cha Ngoswe Penzi Kitovu cha Uzembe, anasema ili mtu awe msanii mzuri katika tasnia ya Sanaa ambayo inakuwa kwa kasi ni lazima apitie mafunzo ili aweze kufanya kazi zake kwa ufanisi na weledi.
Anasema moja kati ya vitu vinavyosababisha kazi nyingi za wasanii kushindwa kufanya vizuri katika soko la kimataifa, ni kutokana na kufanya kazi zao chini ya kiwango kwa kujikita zaidi kwenye biashara (masilahi zaidi) bila ya kuzingatia maudhui ili kazi iwe na ubora unaohitajika.
Vinavyodumaza sanaa
Anasema moja kati ya vitu vinavyosababisha Sanaa ya maigizo kushindwa kufanya vizuri ni kukua kwa teknolojia pia sanaa ya maigizo ni ngumu na ina gharama kubwa ikilinganishwa na sanaa ya nyingine.
Bila kufafanua anasema licha ya teknolojia kuwa nzuri katika ulimwengu wa sasa, lakini kukua kwa teknolojia hiyo kumechangia sanaa ya maigizo ishindwe kufanya vizuri katika soko.
“Kukua kwa teknolojia kumesababisha Sanaa ya maigizo kushindwa kufanya vizuri na hii inatokana na ukweli kwamba sanaa ya maigizo ni ngumu na ina gharama kuliko sanaa nyingine, lakini ndiyo sanaa pekee ambayo mtu akiamua kuifanya anaifanya kwa weledi na ustadi wa juu kwani mtu hawezi kufanya sanaa ya maigizo kama hajapitia darasani,” anafafanua.
Anasema mbali na Sanaa ya maigizo kuwa na gharama kubwa pia mapato yanayotokana na Sanaa za maonyesho ni madogo na hiyo inatokana na watu wanaukuja kutazama au kuangalia maonyesho ya sanaa za maigizo kuwa wachache tofauti na maonyesho mengine.
Nini kifanyike
Anasema ili kukuza tasnia ya sanaa ya maigizo nchini, ni wakati wa kuboresha Sanaa hiyo kuanzia shule za msingi ili kuwa na wasanii wenye utaalamu na hivyo kukuza vipaja na kuongeza ajira kwa vijana.
Anabainisha kuwa tasnia hiyo inatakiwa iunde sera ambayo itatumika shuleni ili kuibua vipaji kupitia somo la sanaa, kwani uwezo wa kufundisha masomo hayo upo na walimu wa masomo ya sanaa ni wengi ikilinganishwa na zamani.
Mbali na kutungwa sera pia jamii iwe na mtazamo chanya kuwa kazi ya sanaa ya maigizo ni kazi kama kazi nyingine, hivyo jamii itoe ushirikiano kwa watoto wanaopata mafunzo ya sanaa na kujiunga katika tansia hiyo.
Wataalamu wanasemaje?
Mratibu wa Mradi wa Kujenga Weledi wa Sanaa za Maonyesho Tanzania, Eliachim Malimi anasema kukosa weledi na uhaba wa elimu ya kutosha kwa watu wanaofanya uandishi wa sanaa za maonyesho ni kikwazo kwa wasanii wengi kushindwa kufanya vizuri kwa tasnia hiyo.
Malimi anasema wasanii licha ya kuwa na vipaji, lakini havisaidii kama hawajapitia mafunzo ambayo ndiyo humfanya msanii kuwa na uwezo wa kubuni na kufanya kazi yake kwa ufanisi na hivyo kuwa uandishi mzuri wa sanaa za maonyesho na tamthiliya.

“Weledi ubunifu na elimu ni vitu vikuu anavyotakiwa kuwa navyo mtu kwenye uandishi wa sanaa za maonyesho na hii itamsaidia msanii aweze kufanya vizuri katika tasnia hii,” anasema Malimi.
Malimi ambaye kwa sasa anatoa mafunzo katika vikundi vitatu vilivyopo chini ya Kampuni ya Parapandani ambavyo ni Sanaa ya maigizo vya Malezi Youth Theather, Lumumba na Parapanda.
Anasema Parapanda ni Kampuni ya Sanaa ya Maonyesho inayojihusisha na sanaa na ina miaka 20 sasa tangu ilipoanzishwa, lengo kuu la kuanzishwa ni kutoa mafunzo ya sanaa kwa watoto wadogo ili kurudisha sanaa ya utamaduni.
Malima anasema lengo la kutoa mafunzo ya sanaa kwa vijana ni kuleta matumaini kwa vijana wadogo katika kazi za sanaa na uandishi wa maonyesho pamoja na tamthiliya.
Anasema mwaka 2012 kampuni hiyo ilifanya miradi mbalimbali ya maendeleo ikiwiwemo miradi ya Shirika la Kazi Duniani (ILO), Matokeo Makubwa Sasa (BRN) na Umoja wa Ulaya ambako walikuwa wanafanya uhamasihaji kupitia sanaa.
“Tumeamua kutoa mafunzo kwa wasanii wetu ili kuwajengea weledi wa kuandika kwa ufasaha tamthiliya na uandishi wa sanaa za maonyesho, ili waweze kupata masoko na kukuza sanaa ya uandishi wa maonyesho,” anasema Eliachim.
Anatolea mfano Kikundi cha Lumumba Theatre kimefanya vizuri katika onyesho la maigizo ya Kinjekitile Ngwale katika vita vya Maji Maji 1905-1907 kupitia kitabu kilichoandikwa na mwandishi na mtunzi mahiri wa vitabu na riwaya nchini, Ibrahim Hussein 1969 na kuchapwa tena 1981.
Malimi anasema kikundi hicho cha Lumumba Theatre kiliamua kufanya sanaa hiyo ya maigizo ya mpiganaji huyu, ambaye alianzisha vita vya Maji Maji wakati wa mapambano dhidi mkoloni wa Kijerumani.
“Kujenga weledi kwa msanii ndiyo nguzo muhimu ili weweze kuandika andishi nzuri la tamthilia litakalomwezesha kuvutia watazamaji au wasikilizaji ili waweze kupata soko la ndani au nje ya nchini kupitia sanaa za ngoma na maonyesho,” anasema.
“Tunatumia mbinu hizo ili kufikisha ujumbe kwa jamii ili iweze kuelewa kwani ujumbe wa sanaa ya maonyesho ndiyo njia rahisi kwa jamii kuweze kuelewa kuliko hata mkutano,” anasema Malimi.
Mmoja wa washiriki wa mafunzo hayo kutoka Kikundi cha Lumumba, Ahmad Madai anasema mafunzo hayo yatamsaidia katika kazi za sanaa ya maigizo kwa sababu hapo awali alikuwa akifanya kazi chini ya ubora kwa kukosa mafunzo.
“Kitu kipya nilichokipata katika mafunzo haya ni namna ya uandishi wa mchezo kwa sababu hapo awali tulikuwa tunacheza bila taaluma, lakini kupitia mafunzo ya darasani sasa sanaa ya maigizo tutaifanya kwa weledi na ubunifu mkubwa,” anasema Madai.

Nini kifanyike
Mandai anasema ili tasnia ya sanaa ya maigizo isonge mbele Serikali haina budi kutoa msaada wa kutosha siyo, kusubiri viongozi wakubwa wa dunia kuja na kuwatafuta wasanii wa ngoma za asili na waandishi wa sanaa za maonyesho bali kujenga uwezo kwenye soko la ndani katika majukwaa.
Kwa nini mafunzo hayo
Mwongozaji wa filamu wa sanaa kutoka Kikundi cha Parapanda Theatre Lab Trust, Amani Lukuli anasema lengo la kutoa mafunzo hayo ni kuvifanya vikundi viwe na utawala mzuri na kuepuka kugawanyika pamoja na kuwa na uwezo wa kuandaa kazi zao wenyewe kupitia bajeti zao na siyo kusubiri wahisani.
Changamoto zilizopo
Lukuli anasema moja kati ya changamoto zilizopo katika tasnia ya sanaa ni kwamba Sanaa za maonyesho zipo chini, lakini kupitia mafunzo hayo wanaweza kupeleka ushawishi kwa jamii hasa baada ya kutumika katika uhamasishaji wa miradi mbalimbali ya maendeleo ya leo
Chanzo:Mwananchi
Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399.

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Kilimanjaro Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa