Home » » ASKOFU SHOO: VIPORO ESCROW VINAUMIZA TUMBO

ASKOFU SHOO: VIPORO ESCROW VINAUMIZA TUMBO

  Askofu Mkuu wa Kanisa la kiinjili la kiluther Tanzania (KKKT), Dk Alex Malasusa (kushoto) akimsimika Mchungaji Dk Fedrick Shoo kuwa Askofu mpya wa KKKT Dayosisi ya kaskazini katika ibada iliyofanyika jana katika usharika wa Moshi mjini.

Askofu mpya wa Dayosisi ya Kaskazini ya Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania (KKKT), Dk Fredrick Shoo jana alitoa ujumbe mzito kwa Rais Jakaya Kikwete alipomtaka kuwawajibisha haraka wahusika kwenye kashfa ya escrow kwa kuwa “viporo vinaumiza tumbo”.
Dk Shoo aliyemrithi askofu Dk Martin Shao aliyestaafu, alitoa kauli hiyo mbele ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais (Utawala Bora), George Mkuchika ambaye alimwakilisha Rais, wakati akihutubia kwenye ibada ya kuwekwa kwake wakfu na kusimikwa kwa msaidizi wake, Mchungaji Elingaya Saria iliyofanyika Usharika wa Moshi Mjini.
Mbali na Waziri Mkuchika, wengine waliokuwapo kwenye ibada hiyo ni mawaziri wakuu wa zamani, Frederick Sumaye na Edward Lowassa, pamoja na Waziri wa Maliasili na Utalii, Lazaro Nyarandu. Pia walikuwapo baadhi ya wabunge na maaskofu wa dayosisi 24.
Katika hotuba yake, Dk Shoo alisema kanisa linasikitishwa na ufisadi mkubwa unaoendelea miongoni mwa viongozi na watumishi wa umma na kiburi wanachokionyesha wanapoelezwa ukweli.
“Kinachotusikitisha zaidi ni wahusika kuonyesha jeuri kubwa na ukakamavu wa hali ya juu pale wanapoambiwa,” alisema Dk Shoo huku akishangiliwa.
“Mimi sioni mantiki kama mtu amehusika katika mambo fulani, halafu anaanza kusema sikueleweka vizuri halafu anajiuzulu.”
Ingawa hakumtaja kwa jina kiongozi huyo, Jaji Fredrick Werema alijiuzulu nafasi yake ya Mwanasheria Mkuu kwa kumwandikia barua Rais akieleza kuwa ushauri wake katika suala la escrow haukueleweka na umesababisha tafrani.
Katika sakata hilo la Escrow, Jaji Werema ndiye anayedaiwa kuandika barua akieleza kuwa fedha zilizokuwa kwenye Akaunti ya Tegeta Escrow zilipwe IPTL bila ya kukatwa kodi.
“Tunatambua Rais ameanza kuchukua hatua dhidi ya watu kama hawa. Tunazidi kumwombea yeye na Serikali yetu ili wamwonyeshe hatua zaidi zinazofaa kuchukuliwa,” alisema Askofu Shoo.
“Panapohitajika kuchukua hatua, tusiweke viporo. Unajua viporo vikishakuwa vya muda mrefu, vinaumizaa tumbo,” alisisitiza Dk Shoo huku umati uliofurika ukilipuka kwa furaha na makofi.
Akitangaza uamuzi wake kuhusu maazimio ya Bunge la Muungano, Rais Kikwete alitangaza kumwondoa kazini Profesa Anna Tibaijuka, aliyekuwa Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, lakini akasema amemweka kiporo Waziri wa Nishati na Madini, Profesa Sospeter Muhongo.

Wanasiasa kujipitisha
Askofu Shoo pia hakuwasitiri wanasiasa wanaopita makanisani na misikitini kutafuta umaarufu ili uwanufaishe kupata madaraka.
“Sisi tunapenda kuwaasa wasaka madaraka kama hao, wanaokimbilia kusaka umaarufu rahisi, tunawatambua na tutawatambua kwa rangi zao,” alisema askofu huyo.
“Ningependa ijulikane kwa wanasiasa na waumini wote kwamba nyumba za ibada ni mahali patakatifu. Si mahali pa kufanyia usanii. Sina maana kila mwanasiasa ni msanii.
“Kanisani ni mahali panapotakiwa kukaribiwa kwa hofu na kwa uchaji. Siyo uwanja wa siasa. Tumpe Mungu yaliyo ya Mungu na ya Kaisari yaliyo ya Kaisari lakini pasipo kuharamisha unabii.”
Kuhusu Panya Road
Katika hatua nyingine, Askofu Shoo alisema kuibuka kwa kundi la wahalifu maarufu kama Panya Road jijini Dar es Salaam ni matokeo ya vijana wengi nchini kukosa ajira.
“Ajira kwa vijana ni changamoto kubwa kutokana na kufungwa kwa viwanda vingi vilivyokuwapo, matokeo yake wengi wanaokaa bila ajira, wamejiingiza katika ajira zisizofaa,” alisema.
Dk Shoo alisema kama hali ya vijana wengi kukosa ajira itaendelea kama ilivyo sasa, itakuwa ni hatari kubwa kwa usalama wa nchi na kuonya kuwa watu waliokata tamaa ni vigumu kuwatawala.
“Watu watakata tamaa na watu waliokata tamaa hawatawaliki. Tukiendelea hivi tusishangae hao wanaoitwa Panya Road wakajitokeza hata hapa Moshi, Mkoa wa Kilimanjaro,” alisema.
Askofu Shoo alisema Tanzania si masikini na kwamba nchi imejaliwa utajiri mwingi na kusisitiza kuwa wanaosema Tanzania ni maskini na kuamini hivyo, ni maskini wa fikra
“Tunachohitaji ni viongozi na watumishi wenye roho ya uzalendo. Bila hivyo ni vigumu kuhakikisha kuwa rasilimali za nchi hii zinawanufaisha Watanzania wote,” alisema.
Mkuchika ajibu
Akijibu hotuba hiyo iliyoonekana kuwa mwiba mkali kwa Serikali, Mkuchika alisema Serikali imekwishachukua hatua na itaendelea kuchukua hatua dhidi ya watu wote waliohusika na sakata la escrow.
“Tayari wahusika wamechukuliwa hatua. Mfano Mwanasheria Mkuu wa Serikali amejiuzulu na Waziri mmoja ameondolewa katika Baraza la Mawaziri,” alisema Mkuchika katika hotuba yake.
Mkuchika alisema hata Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati na Madini, Eliakim Maswi amesimamishwa kazi ili kupisha uchunguzi na kwamba uchunguzi dhidi ya watu wengine waliotajwa bado unaendelea.
“Kwa wale wengine ambao uamuzi bado haujafikiwa, vyombo vya dola, kama (Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa) Takukuru na Sekretarieti ya Maadili ya Viongozi wa Umma, vinavifanyia kazi,” alisema.
Mkuchika alimpongeza Askofu Shoo kwa kutambua tatizo la wanasiasa kutumia makanisa na misikiti kunadi sera zao, lakini akawashauri viongozi wa dini kutowakaribisha wanasiasa hao ili kukomesha hali hiyo.
“Endapo viongozi wa dini watakataa, tatizo hili halitakuwepo. Msiwakaribishe kutumia maeneo ya kanisa na misikiti kuhubiri siasa. Tusichanganye dini na masuala ya siasa,” alisisitiza Mkuchika.
Dk Malasusa atoa angalizo
Mkuu wa Kanisa la KKKT, Dk Alex Malasusa alisema mwaka 2015, nchi ina mambo mengi, lakini ni vyema Serikali ikaweka kipaumbele katika mambo muhimu zaidi, likiwamo Daftari la Wapigakura.
“Serikali iboreshe Daftari la Wapigakura ili wananchi wengi waweze kujiandikisha na kupiga kura. Mnasema tuendeleze amani lakini amani haiwezi kuwepo kama haki haipo,” alisema.
Askofu Malasusa pia alitahadharisha kuibuka kwa vikundi vya uhalifu kama Panya Road na kudokeza kuwa Moshi kumeibuka kundi la Kanyaga Twende.
Dk Malasusa alimwambia Mkuchika kuwa suala la utawala bora si la Rais, bali ni la kwake na kumtaka asimamie utawala wa sheria vinginevyo, mwisho wa kuibuka vikundi hivyo utakuwa mbaya.
Chanzo:Mwananchi
Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399.

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Kilimanjaro Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa