Home » » SERIKALI YATAKA TAARIFA KUPUNGUA MAJI MLIMA KILIMANJARO.

SERIKALI YATAKA TAARIFA KUPUNGUA MAJI MLIMA KILIMANJARO.

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 

SERIKALI mkoani Kilimanjaro imetaka Hifadhi ya Taifa ya Mlima Kilimanjaro (Kinapa) kwa kushirikiana na Ofisi ya Maji ya Bonde la Pangani (PBWO), kuandaa taarifa za kitaalamu zinazoonesha jinsi mlima huo ulivyopunguza maji yake kwenda katika mabwawa ya kuzalisha umeme.
Mlima Kilimanjaro umetajwa kama chanzo kikuu cha maji katika bwawa la Nyumba ya Mungu na Hale mkoani Tanga ambayo kwa pamoja hutumika kwa ajili ya kuzalisha umeme.
Katika taarifa iliyotolewa na Ofisa Habari wa Mkoa wa Kilimanjaro, Shaban Pazi, inaeleza Mkuu wa Mkoa huo, Said Meck Sadiki alisema hayo baada ya kupokea taarifa ya Mhifadhi Mkuu wa Kinapa, Beitrita Loibooki aliyekuwa akielezea taarifa ya maendeleo ya hifadhi hiyo na changamoto zake.
“Pamoja na taarifa yako inayoonesha kwamba mlima huu unachangia zaidi ya asilimia 80 ya maji katika mabwawa hayo... bado hili ni jambo la kulitazama kwa jicho la pili, nipeni taarifa ya kitaalamu inayoonesha maji yatokayo mlima Kilimanjaro kwenda katika mabwawa hayo yamepungua kwa kiasi gani,” alisema.
Alisema kutolewa kwa taarifa hiyo kutatoa picha halisi ya jinsi athari za uharibifu wa mazingira na mabadiliko ya tabianchi kunavyoweza kuathiri mazingira na namna gani inaweza kuathiri shughuli za kiuchumi.
Alisema taarifa hiyo pia itaonesha jinsi kupungua kwa maji katika mlima Kilimanjaro unavyoweza kuathiri vyanzo vya maji na mito, jambo litakalosababisha upungufu wa maji majumbani na viwandani na kuathiri maisha ya kila siku.
Kwa upande wake, Mhifadhi wa Kinapa, Loibooki alisema mlima huo unachangia maji katika mabwawa hayo ya kuzalisa umeme kwa asilimia 80 na kwamba kama mazingira ya mlima huo hayatatunzwa ipasavyo upo uwezekano wa mabwawa hayo yakashindwa kuzalisha umeme kama ilivyotakiwa.
CHANZO: HABARI LEO

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Kilimanjaro Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa