Home » » Wanaume 200 wadaiwa kutelekeza familia

Wanaume 200 wadaiwa kutelekeza familia

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 

ZAIDI ya wanaume 200 wamezikimbia familia zao na kuziacha katika hali duni na kwenda kusikojulikana kwa kisingizio cha kukosa shughuli za kiuchumi baada ya kufungwa kwa Bwawa la Nyumba ya Mungu wilayani Moshi.
Kutokana na hali hiyo, baadhi ya wanawake wamedai watoto wao wapo hatarini kukatisha masomo kutokana na kukosa chakula, mahitaji ya shule zikiwemo sare.
Wakizungumza na Mkuu wa Wilaya ya Moshi, Kippi Warioba katika mkutano wa hadhara uliofanyika katika Kijiji cha Mikocheni, Kata ya Arusha Chini, wanawake hao Asha Ndive na Sakina Abdallah walidai maisha yamekuwa magumu.
"Tangu serikali imelifunga bwawa hili Julai mosi, hali ya kiuchumi imekuwa mbaya na wanaume wametukimbia, tumebaki wenyewe na watoto... mkuu wa wilaya tusaidie chakula ili angalau tumudu haya maisha wakati tukitafuta shughuli nyingine,” alisema Asha.
Kwa upande wake, Mwenyekiti wa kijiji hicho, Koromo Kweinasi pamoja na kukiri kukimbia kwa wanaume hao, ameomba serikali kuainisha mipaka ya bwawa hilo ili wananchi wafahamu eneo halisi kwa ajili ya shughuli za kibinadamu.
“Serikali imefunga bwawa, imekataza ufugaji na kilimo pembezoni mwa bwawa, lakini wakati mwingine tunafanya haya bila kujua, tunaomba mipaka ya bwawa iainishwa ili nasi tuiheshimu vinginevyo tutaadhibiwa kila siku,” alisema Kweinasi.
Alisema kijiji hicho chenye kaya zaidi ya 3,894 zinahitaji msaada wa chakula kwani hapo awali walikuwa wakitegemea shughuli za uvuvi pekee na sasa serikal imezisitisha.
Akijibu kauli za wananchi hao, Kippi alitaka mtendaji wa kata kuandaa takwimu za idadi ya kaya zinazohitaji msaada wa chakula na makisio ya mahitaji halisi ili serikali itoe.
Alisema msimamo wa serikali juu ya kusitisha uvuvi upo pale pale lakini akataka wananchi kuuheshimu ili ijaribu kulegeza masharti kulingana na mazingira yatakavyorejea katika hali yake.
Chanzo Na Habari Leo

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Kilimanjaro Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa