Home » » MAKALA: WATANZANIA TUJIFUNZE KUTOKA USANGI,MKOANI KILIMANJARO

MAKALA: WATANZANIA TUJIFUNZE KUTOKA USANGI,MKOANI KILIMANJARO

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399.

 Mwonekano wa baadhi ya nyumba katika moja ya vijiji kata ya Usangi,nyumba hizo zimejengwa milimani lakini miundombinu ya umeme imewafikia
Huu ni mradi wa maji uliopo katika kijiji cha Kirogwe kata ya Usangi,hiki ni kipimo kinacho onesha maendeleo katika kijiji Hicho


Imeandaliwa na Abeid Othman
Hivi karibuni,  nilifanya ziara ya siku kadhaa katika kata ya Usangi iliyopo Wilaya ya Mwanga mkoani Kilimanjaro.

Ni ziara iliyoratibiwa na asasi ya Twaweza kwa minajili ya kupata picha halisi ya maisha ya Watanzania wa kada za chini.

Kupitia ziara hiyo,  nilipata fursa ya  kuwa karibu na Watanzania wa vijijini, huku nikijifunza kwao kuhusu Wanachofikiri na  wanachotamani   kwa ustawi wa maisha yao na maendeleo ya nchi kwa jumla.

Ukiondoa kujichanganya kwangu na wananchi hao, ziara ya Usangi ilinifunza mengi ambayo kwa kuandika makala haya, pengine Watanzania wenzangu tunaweza kujifunza kutoka huko.

Kimsingi, vijiji vya Usangi na pengine mkoa mzima wa Kilimanjaro vina tofauti kubwa ya kimaendeleo, ukilinganisha na vijiji vingi katika maeneo mbalimbali ya nchi yetu. Usangi na mkoa mzima kwa jumla, kuna watu  wanaokumbuka kuendeleza kwao.

Wenyeji wa Usangi  wanatambua asili  yao; wanajua walikotoka ndio maana wengi  huamua kurudi kwao kila mwisho wa mwaka. Ni dhahiri kuwa wanarudi katika maeneo waliyoyaendeleza; wanajua pa kufikia kama familia.

Nilichokiona huko  ni kuwapo kwa nyumba nyingi za kifamilia tena zikiwa sehemu moja. Huu ni utamaduni unaopaswa kuigwa na watu wengine.

Nilikuwa nasikia taarifa za umeme kufika mpaka kwenye mashamba ya migomba, hili nimeliona kwa macho yangu.
 Kama haitoshi, kuna miundombinu ya maji ya bomba hadi maeneo ya milimani. Yote haya ni kwa sababu ya kuwapo kwa wawakilishi wa wananchi wanaojitambua na mwamko wa wakazi wake.

Wasomi wao nao walisoma na kuamua kurudi nyumbani kuendeleza; hawakusoma ili wajitenge na watu washamba vijijini mwao.

Ukifika Usangi  kwa mfano, ni rahisi kujuzwa kuwa hapa ni kwa mzee David Msuya (Waziri Mkuu Mstaafu,  pale kwa kina Asha- Rose  Migiro (Waziri katika serikali ya awamu ya nne) na  viongozi wengine  wengi wastaafu na walio madarakani.

Kwa sababu  ya umakini wa wakazi, kijiji kama Kirongwe  nilichoishi kwa siku kama  tatu hivi  na vingine vya jirani  vimeendelea kiasi cha kuvifananisha na mji mdogo.

 Katika  vijiji  hivi nimeshuhudia ujenzi wa nyumba za kisasa yakiwamo maghorofa, usafiri wa kuaminika. Haya ni muhali kuyakuta katika vijiji vingi nchini. Miaka ya nyuma, nilifanya ziara katika kijiji  cha Lula Kawala mkoani Rukwa.

Nilikuta shule ya kijiji ikiwa haina  madawati, huku wanafunzi wakirundikwa darasani  kama matenga ya viazi.Cha  ajabu, mita chache kutoka shuleni kulikuwa na  shamba kubwa la miti ya mbao.

Halikuwa shamba la mwekezaji kutoka nje, bali la watu ambao ni wazaliwa wa eneo hilo, lakini hawakuona haja ya kutumia rasilimali hiyo kwa ajili ya kuwanusuru watoto wao.  Naamini hili haliwezi kutokea mkoani Kilimanjaro.

Najua wapo wanaoweza kunikosoa kwa kudai Usangi na hata wilaya nzima ya Mwanga, imeendelea kwa sababu ya kuwapo kwa viongozi waliojipendelea kupeleka maendeleo huko walipokuwa madarakani.
Pengine kuna ukweli, lakini nchi hii imekuwa ikitoa viongozi karibu kila kona, mbona haya ya Usangi hatuyaoni mahala pengine, au kutoendeleza kwako ndio uzalendo?

Tofauti na viongozi wa Kilimanjaro wanaorudi kwao kuendeleza, uko ushahidi wa viongozi mbalimbali  wanaokimbia maeneo yao ya asili.
Wanaona aibu kurudi makwao, ndio maana wengi wamejenga makazi ya kifahari nje ya maeneo yao ya asili.  Hili halipo Moshi, ndio maana mtu anaweza kujenga ghorofa lenye hadhi  kijijini.

Nasi  wengine tuige, tuishi mijini lakini tukumbuke kuendeleza tulipotoka.

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Kilimanjaro Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa