Home » » MAKALA: "NILIYOYAONA WILAYA YA MWANGA YAKANIVUTIA"

MAKALA: "NILIYOYAONA WILAYA YA MWANGA YAKANIVUTIA"

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399.


 Mfano wa nyumba zilizojengwa milimani

Shughuli ya kubeba kuni kutoka chini kwenda mlimani ilipo nyumba ikiendelea

Abeid Poyo



Kutembea sana ni kujua mengi. Na kwa hakika kama wahenga walivyosema: ‘mtembea bure sio sawa na mkaa bure.’


Ukweli ni kuwa unaweza kutembea ukaokota kitu kikakufaa maishani.


Hiki ndicho kilichonitokea mimi, shukrani kwa asasi makini ya Twaweza ambayo mwezi Mei mwaka huu, iliniwezesha kwa mara ya kwanza kukanyanga ardhi ya wilaya ya Mwanga iliyopo mkoani Kilimanjaro. 


Ni ziara ya siku kadhaa iliyonichukua katika vijiji kadhaa hasa kijiji cha Kirongwe kilichopo kata ya Usangi.


Nikiwa Usangi ndipo nilipoona mengi yaliyonivutia ambayo Watanzania wanapaswa kujifunza kutoka huko. 


Mambo kadhaa yalinivutia ikiwamo ujenzi wa nyumba za milimani. Ikumbukwe huku kuna maeneo makuu mawili viko vijiji vya chini (low land) kama  na vile vya juu (high land) kama .


Wakati makazi kwa wale wanaoshi chini ya milima ujenzi wake ni rahisi, wapo wanaojenga milimani.


Siyo kazi rahisi lakini simulizi za wenyeji zinasema wapo watu maalumu wenye utaalamu wa kuchonga miamba na hatimaye kupata kiwanja mlimani.


Huko nyumba itajengwa, kama umeme utafika, maji pia na kama ni bustani au hata shamba utaliona.


Nikiwa katika kijiji cha Kirongwe, mwenyeji wangu ambaye pia ni Mwenyekiti wa kijiji, Mzee Nasibu Ramadhani, amejenga nyumba yake mlimani, kibarua kikawa kwangu mimi na mwenzangu Richard Temu kupanda na kushuka kila siku, haikuwa kazi rahisi lakini tukazoea na wakati mwingine tulilazimika kupandisha kuni kutoka chini ya mlima kupeleka mlimani ilipo nyumba kwa ajili ya matumizi ya familia. (Angalia picha mwenzangu, Richard akiwa na kuni akipandisha mlimani).


Wilaya ya Mwanga hasa vijiji nilivyobahatika kutembelea vinavutia kwa ukijani wake, na haya yote tisa, umeshaona umeme ukipita hadi kwenye mashamba ya migomba? Huku maendeleo yalishafika siku nyingi, ndio maana sio ajabu kuona hata migombani kuna nguzo za umeme.


Hii ni wilaya ambayo wakazi wake wa asili ni Wapare. Naam nilichovutika huko ni ukarimu wa wenyeji. Mpare humwambii kitu kwa chai. Katika nyumba nyingi tulizotembelea aghalabu makaribisho yaliambatana na kupewa chai. Pata picha unatembelea nyumba nne au tano ndani ya saa mbili na kila nyumba lazima unywe chai! Ukarimu huu ni wa aina yake.


Nilielezwa kuwa chai ni sehemu ya maisha ya Wapare, huo ni utamaduni wao.


‘’Yaani ndio desturi yetu, tena siku hizi watu hawana ng’ombe, ungepewa chai ya maziwa tu kila nyumba au chakula hadi jasho likutoke, anasema mwenyeji mmoja wa Usangi aitwaye Asiatu Msuya.


Pamoja na yote haya niliyojionea upareni, kitu kimoja kilinishangaza. Awali nilikuwa nikijua kuwa makande ndicho chakula mojawapo kikuu cha huko. Ajabu ni kuwa katika siku zote nilizokaa Usangi hasa kijiji cha Kirongwe, sikuona makande mezani.


Nilipomuuliza mwenyeji mwingine wa hukao aitwaye Ziada Kejo, alinijibu: ‘’ hapana, ni mara chache (kula makande). Chakula kikuu ni ndizi au kishumba.



Kishumba kwa mujibu wa Ziada ni mchanganyiko wa maharage na ndizi. Hiki ni moja ya vyakula vya Upareni kama ilivyo kwa kirembwe.  Hata hivyo siku zangu chache za kukaa Usangi, sikubahatika kula kishumba, pengine safari ijayo panapo majaliwa, nitaomba wenyeji wangu wanipikie kishumba.


Abeid Poyo ni mwandishi wa masuala ya kijamii na maendeleo. 0754990083

 

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Kilimanjaro Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa