Home » » MADARAKA: MFUMO WA ELIMU UREKEBISHWE

MADARAKA: MFUMO WA ELIMU UREKEBISHWE

na Rodrick Mushi, Moshi
MTOTO wa Baba wa Taifa, Madaraka Nyerere, ameshauri mfumo wa elimu nchini kufanyiwa marekebisho vinginevyo taifa litaendelea kuwa na wasomi wasiokuwa na sifa.
Amesema mfumo wa elimu unatakiwa kuangaliwa upya kuanzia elimu ya msingi hadi vyuo, ili taifa liweze kuzalisha wahitimu wenye elimu bora.
Madaraka alitoa kauli hiyo mwishoni mwa wiki kwenye mahafali ya sita ya kidato cha nne ya Shule ya Sekondari Sungu iliyoko wilaya ya Moshi Vijijini, mkoani Kilimanjaro.
Alisema kama serikali inavyoita ukimwi kuwa ni janga la taifa, hata sekta ya elimu imegeuka janga la taifa na kwamba inahitaji kufanyiwa maboresho na mapambano ikiwa ni pamoja na kutenga bajeti ya kutosha.
“Kumaliza tatizo la elimu sio suluhisho la muda mfupi, kwani inatakiwa kufumuliwa kabisa kwa mfumo mzima wa elimu na kuhakikisha wanafunzi wanakuwa na sifa kwa sababu unaweza kukutana na mhitimu wa Chuo Kikuu mpaka unajiuliza amehitimu namna gani elimu hiyo kwani unakuta hana sifa,” alisema.
Kwa upande wake, mkuu wa shule hiyo, James Thomas, alisema wananchi wa eneo hilo wamekuwa wakitoa ushirikiano mkubwa kwenye suala la kuchangia elimu na ndiyo maana shule hiyo imekuwa na maendeleo mazuri.
Pamoja na hayo, alisema shule hiyo inakabiliwa na changamoto mbalimbali ikiwamo ukosefu wa maabara, maktaba pamoja na bwalo la kulia chakula kwa wanafunzi.
Chanzo: Tanania Daima

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Kilimanjaro Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa