Home » » MAOFISA TRA HOLILI KATIKA KASHFA YA RUSHWA

MAOFISA TRA HOLILI KATIKA KASHFA YA RUSHWA

na Charles Ndagulla, Moshi
MAOFISA wa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) katika kituo cha Forodha cha Holili wameingia katika kashfa wakihusishwa na upokeaji rushwa ya mamilioni ya fedha kutoka kwa wafanyabiashara wanaojihusisha na usafirishaji wa sukari kwenda nchini Kenya kwa njia za magendo.
Uchunguzi uliofanywa na Tanzania Daima Jumatano umefichua mipango yote inayofanywa na maofisa hao wakishirikiana na wafanyabiashara wa magendo ya sukari kuikosesha serikali mamilioni ya fedha.
Gazeti hili katika uchunguzi wake limebaini kuwa kabla ya wafanyabiashara hao kuvusha shehena ya sukari kwenda nchini Kenya ambako inaaminika kumekuwapo na uhaba wa sukari, hufanya vikao vya kuweka makubaliano ya kiwango cha rushwa kitakachotolewa na wafanyabiashara hao.
Inadaiwa kila gari moja aina ya Fuso Tandamu maofisa hao wenye dhamana ya kukusanya kodi kwa niaba ya serikali, hupokea wastani wa sh 300,000 na 500,000 kulingana na makubalino baina ya mfanyabiashara anayesafirisha sukari.
Kwa muda wa wiki moja sasa wastani wa magari 10 hadi 15 yamekuwa yakisafirisha sukari kila siku kutoka mji mdogo wa Himo kwenda nchini Kenya kupitia njia ya kwa Mandara hadi eneo kunakochimbwa mchanga aina ya Pozolana wilayani Rombo kabla ya kuingia nchini Kenya kupitia njia za panya.
Kazi hiyo ya kusafirisha sukari kwenda nchini Kenya kwa njia za magendo hufanikishwa na askari mgambo waliopo eneo la kwa Hussen nje kidogo ya mji mdogo wa Himo ambapo jukumu lao ni kuhakikisha wanasindikiza magendo hayo hadi mpakani mwa Kenya na Tanzania.
Mmoja wa mgambo hao aliyeomba jina lake lisitajwe kwa hofu ya kupoteza kibarua chake, alimeliambia Tanzania Daima Jumatano kuwa wamekuwa wakilipwa ujira wa kati ya sh 30,000 hadi sh 50,000 kwa kusindikiza magari yaliyosheheni sukari.
Kwa mujibu wa uchunguzi wetu biashara hiyo ya magendo ya sukari imewawezesha mgambo wengi katika ukanda huo wa Holili na Himo kuwa na kipato kikubwa huku baadhi yao wakifanikiwa kujenga nyumba za kisasa pamoja na kununua magari ya aina mbalimbali.
Wengine ambao wamekuwa wakinufaika na biashara hiyo ya magendo ya sukari ni askari wa kituo cha polisi Himo ambao hupokea rushwa ya wastani wa sh 500,000 hadi 700,000 kwa kila gari, rushwa ambayo imepewa jina la ‘safisha njia’.
Uchunguzi umebaini kuwa askari hao pamoja na maofisa wa TRA, huyaondoa magari yao ya doria kwenye barabara ambazo hutumika siku ya kusafirishwa kwa sukari hiyo na kwenda kupiga doria eneo jingine lengo likiwa ni kuruhusu shehena za sukari kupita bila woga.
Hata hivyo, meneja wa TRA mkoani Kilimanjaro, Patience Minga, hakuwa tayari kujibu ujumbe mfupi wa maandishi aliotumiwa na mwandishi wa habari hizo kutaka ufafanuzi juu ya tuhuma zinazowakabili maofisa wake.
Pamoja na mwandishi kutuma ujumbe mfupi wa maandishi kupitia simu ya kiganjani, jana pia hakuwa tayari kupokea simu ya mwandishi wa habari hizi na kila ilipopigwa iliita bila kupokelewa.
Chanzo: Tanzania Daima

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Kilimanjaro Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa