Home » » MBARONI KWA KUIHUJUMU TANESCO

MBARONI KWA KUIHUJUMU TANESCO



Na Upendo Mosha, Hai
SHIRIKA la Umeme Tanzania (TANESCO) mkoani Kilimanjaro, linawashikilia watu saba kwa tuhuma za kuhujumu miundombinu ya umeme, jambo ambalo ni hatari kwa maisha ya watu na linaloweza kusababisha vifo.

Akizungumzia tukio hilo la kukamatwa kwa watu hao, Meneja wa TANESCO wilayani Hai, James Chinula, alisema kukamatwa kwa watu hao kumetokana na msako mkali uliofanywa katika wilaya hiyo katika vijiji vya Machame, Masama na Hai mjini.

Alisema watu hao walikamatwa baada ya kugundulika kujiunganishia umeme isivyo halali kwa kupitisha waya katika nguzo na kisha kuchimbia chini ya ambao ambapo waya hizo zimechubuka, jambo ambalo alisema ni hatari kwa maisha ya watu.

Aliwataja watu hao kuwa ni Ally Omary, Stephano Eliafiye, Yohana Zacharia, Arnold Jonas, Shani Ulomi pamoja na Sharifa Ally, wote wakazi wa Hai.

Vitendo vya kuhujumu miundombinu ya umeme vimekuwa vikishamiri mkoani hapa na kwamba baadhi ya watu pia wamekuwa wakichangia ukatikaji wa umeme mara kwa mara na kusababisha shirika hilo kutupiwa lawama.

“Operesheni hii tumefanikiwa kukamata watu saba na hii ni muendeleo wa msako unaofanywa nchi nzima na wilaya yetu ni miongoni mwa wilaya zenye changamoto ya tatizo hili jambo ambalo limekuwa likitusumbua sana katika utoaji wa huduma zetu,” alisema.

Chinula aliwataka wananchi kushirikiana na shirika hilo kufichua uhalifu wa wizi wa umeme na kwamba kufanya hivyo kutapunguza matukio ya vifo na ukatikaji wa umeme wa mara kwa mara wilayani hapa

Chanzo: Mtanzania

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Kilimanjaro Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa