Home » » MFUMO DUME WAPUNGUA

MFUMO DUME WAPUNGUA



na Rodrick Mushi, Rombo
TATIZO la mfumo dume kwa baadhi ya wazazi wilayani hapa limeelezwa kupungua, hususani katika kutoa fursa sawa katika kuwapatia watoto wa kike na wa kiume elimu pamoja na kurithi mali.
Kipindi cha nyuma Rombo ilikuwa miongoni mwa wilaya zilizokuwa zikikabiliwa kwa kiwango kikubwa na mfumo dume, ikiwemo watoto wa kike kutokuwa na haki ya kumiliki ardhi pamoja na elimu.
Mkuu wa Shule ya Sekondari Shauritanga iliyopo wilayani hapa, inayomilikiwa na Jumuiya ya Wazazi wa CCM, Kalisti Shirima, akizungumza kwenye mahafali ya kidato cha nne, alisema kuwa tatizo hilo lilichangiwa na umaskini kwa kiwango kikubwa.
“Mfumo dume kipindi cha nyuma ulikuwa unasumbua maana nilikuwa napata matatizo hayo kwa wanafunzi wa kike ambao wazazi wao walikuwa hawataki kuwalipia ada, lakini baada ya wananchi wengi kuwa na uwezo wa kifedha, tatizo hilo limepungua,” alisema.
Pamoja na umaskini, alisema pia hatua ya wananchi kuelimika pamoja na kujua umuhimu wa kutoa elimu kwa watoto wote na kuwarithisha mali bila kubagua imesaidia.
Kwa upande wake Kaimu Katibu tawala wilayani Rombo, Yusuph Kasuka, aliyekuwa mgeni rasmi kwenye mahafali hayo, alisema kuwa jamii inatakiwa kuondokana na vitendo hivyo vya ubaguzi wa kijinsia.
Alisema kuwa sera ya elimu inaeleza kuwa mwanafunzi ambaye ana umri wa kuanza shule anatakiwa kuwepo shuleni, lakini wazazi ambao wamekuwa wakikiuka sheria hiyo ni vyema wakapewa elimu, na kama wanakiuka basi sheria zichukue mkondo wake.
Kasuka alisema sekta ya elimu bado inakabiliwa na changamoto mbalimbali, ikiwemo elimu ya vitendo ambapo jitihada zaidi zinahitajika kwa wadau na serikali kuweza kumudu ushindani wa soko la pamoja la Afrika Mashariki.
Chanzo: Tanzania Daima

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Kilimanjaro Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa