Home » » UCHAGUZI CCM WAENDELEA WILAYANI HAI, WAGOMBEA WANAOTUMIA RUSHWA ILI WACHAGULIWE WAONYWA

UCHAGUZI CCM WAENDELEA WILAYANI HAI, WAGOMBEA WANAOTUMIA RUSHWA ILI WACHAGULIWE WAONYWA

Na Florah Temba, Moshi-Kilimanjaro Yetu


CHAMA cha mapinduzi (CCM) mkoani Kilimanjaro, kimewataka wagombea wa nafasi mbalimbali za uongozi ndani ya Chama hicho, kuacha kuwarubuni wanachama kwa kuwapa rushwa ili wawachague, kwani kufanya hivyo ni kwenda kinyume cha taratibu na kutasababisha kupatikana kwa viongozi wasio waadilifu.

Rai hiyo imetolewa na katibu wa chama hicho mkoani Kilimanjaro Bw. Steven Kazidi, wakati akizungumza na waandishi wa habari ofisini kwake kuhusiana na mchakato wa uchaguzi ndani ya chama hicho mkoani humo.

Bw. Kazidi alisema chama hicho hakitavifumbia macho vitendo vya rushwa katika uchaguzi, na kwamba mgombea yeyote atakayebainika kushinda kwa kutoa rushwa, ataadhibiwa kwa kanuni za chama ikiwemo kunyang’anywa ushindi wake ili kuweza kuwa fudisho kwa watu wengine wenye tabia kama hizo.

“Nitoe wito kwa wagombea wote katika mkoa huu, waache kutoa rushwa ili wachaguliwe, kwani hali hiyo ni kinyume cha taratibu za chama na hatutavifumbia macho vitendo hivyo” alisema Kazid.

Aidha Bw. Kazidi aliwataka pia wanachama wa chama hicho kuwachagua viongozi ambao ni waadilifu,waaminifu  na wachapakazi ambao watakijenga chama na si kukibomoa ikiwa ni pamoja na kuhakikisha wanawaepuka viongozi wanaohitaji madaraka kwa vigezo vya rushwa.

Alisema viongozi wanaotaka kununua uongozi kwa rushwa hawafai kutokana na kwamba uongozi haununuliwi hivyo ni vema wanachama wakawaepuka na kuhakikisha hawawachagui.

Katika mkoa wa Kilimanjaro uchaguzi ulianza jana  Octoba Tatu katika wilaya ya Same,Mwanga na Rombo,ambapo katika wilaya ya Mwanga Mathew Msofe  ametetea kiti chake cha uenyekiti kwa kupata kura  527, huku kiti cha NEC kikichukuliwa na Anania  Tadayo ambaye aligombea ubunge mwaka 2010 na kupata kura 41.

Uchaguzi huo unaendelea leo Octoba 4, wilaya ya Hai, Octoba Tano Moshi mjini, na octoba 12 utafanyika katika wilaya ya Siha na Moshi Vijijini.

Ngazi ya mkoa uchaguzi huo utafanyika Octoba 15  ambapo utamchagua mwenyekiti wa Mkoa na wajumbe wa halmashauri kuu ya mkoa ambapo wagomnbea wa nafasi ya mwenyekiti ni Mildred Kisamo,James Kombe,Idd Juma na Thomas Ngawaiya.

Blogzamikoa

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Kilimanjaro Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa