Home » » Hali mpakani na Holili bado tete

Hali mpakani na Holili bado tete



HALI  bado si shwari katika mpaka wa Tanzania na Kenya katika kituo cha Forodha cha Holili, baada ya wafanyabiashara wa Tanzania kupinga hatua ya serikali ya Mkoa wa Kilimanjaro kushinikiza kufutwa vibali vyao vya kusafirisha mazao kwenda nchini Kenya.
Novemba mosi mwaka huu Wizara ya Kilimo, Chakula na Ushirika ilifuta vibali vya wafanyabiashara wa Tanzania kusafirisha mazao ya nafaka kwenda nchini Kenya lakini Kamati ya Ulinzi na Usalama ya mkoa, iliiteua Kampuni ya Kilimanjaro Uchumi kuchukua jukumu hilo, hatua ambayo ilipingwa vikali na wafanyabiashara hao.
Kutokana na hali hiyo, juzi na jana hali haikuwa nzuri katika mpaka huo kutokana na tishio la wafanyabiashara wa Tanzania kutaka kuzuia magari ya Kenya yasiingie nchini kupakia mazao ya nafaka.
Juzi magari sita yaliyokuwa yamesheheni mazao ya nafaka yakiwa na namba za usajili za nchini Kenya, yalizuiliwa upande wa Tanzania kwa saa sita na polisi wenye silaha kutokana na agizo la Kamati ya Ulinzi na Usalama kuwazuia wafanyabiashara wasipeleke mazao hayo nchini Kenya.
Wakizungumza na waandishi wa habari katika kituo hicho cha Forodha cha Holili, wafanyabiashara hao wamemshutumu Mkuu wa Mkoa wa Kilimanjaro, Leonidas Gama, kwa madai ya kuibeba kampuni hiyo.
Wafanyabiashara hao wamelalamika kuwa uamuzi huo utawaumiza na wanaweza wakajikuta kwenye wakati mgumu na vyombo vya fedha kutokana na kushindwa kurejesha mikopo waliyopata benki.
Kwa upande wake Mkuu wa Mkoa wa Kilimanjaro, Gama, jana alipuuza shutuma hizo na kudai kuwa kuna watu wachache ambao hawataki kufuata taratibu zilizowekwa na kwamba wachache hao wana sababu zao binafsi.
Hata hivyo mkuu huyo wa mkoa alisema kampuni hiyo imeteuliwa na Kamati ya Ulinzi na Usalama ya mkoa kwa lengo la kukusanya mapato katika mpaka huo na kudhibiti mianya ya ufujaji wa mapato.
Mwezi Septemba na Oktoba  mwaka huu Wizara ya Kilimo, Chakula na Ushirika ilitoa kibali kwa kampuni za Kisongo Grain Market, Osaka Stores na Abdilah Mkilindi  kusafirisha mazao ya nafaka kwenda nchini Kenya, kibali ambacho muda wake ulikuwa umalizike Desemba 30, mwaka huu.

Chanzo;Tanzania Daima

1 comments:

Unknown said...

Wafanyabiashara kwa ajili ya masoko ya EAC,SADC,COMESA,AGOA,nk wanakaribishwa kujiunga Tanzania Exporters Association (TANEXA) kwa ajili ya
kujenga nguvu ya pamoja ili kupata uwezeshaji wa kukabiliana na changamoto zinazoizunguka sekta hii muhimu kiuchumi
Email:info@tanexa.com
www.tanexa.com
Blogu:tanexa.blogspot.com

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Kilimanjaro Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa