Home » » TBS yateketeza marobota ya mitumba

TBS yateketeza marobota ya mitumba

SHIRIKA la Viwango Tanzania (TBS) kwa kushirikiana na Jeshi la Polisi, limeendesha operesheni maalumu katika masoko makubwa ya nguo za mitumba katika miji ya Moshi na Arusha yanayodaiwa kuwa wauzaji wakuu wa nguo za ndani zilizopigwa marufuku.
Operesheni hiyo iliyoanza katika masoko ya Klolotoni na soko la Kati na Unga Limited ya jijini Arusha, ilifanyika pia juzi katika masoko ya Meimoria na Mbuyuni ambapo robota zaidi ya tano zilikamatwa na kisha kuteketezwa katika dampo la Kaloleni.
Ofisa Viwango na Mkaguzi mwandamizi wa shirika hilo, Paul Manyilika akizungumza muda mfupi baada ya kuihitimisha zoezi hilo mjini hapa, alisema zoezi hilo litakuwa endelevu kutokana na baadhi ya wafanyabiashara kukaidi agizo la serikali.
“Nguo hizo zina madhara kwa afya ya binadamu na bahati mbaya wengi wetu tunashindwa kutafsiri nini maana ya nguo ya ndani. Nguo ya ndani ni pamoja na chupi, sidiria na soksi na nguo za kulalia ambazo kwa ujumla wake zote hizi zimepigwa marufuku,” alisema Manyilika.
Alisema marobota ya nguo hizo yaliyonaswa na TBS katika operesheni ya kushtukiza iliyofanyika mjini Moshi yameteketezwa na maofisa wake chini ya ulinzi wa polisi na kwamba wahusika hao kwa sasa wanafanyiwa mahojiano, ili kubaini watu hao wanaingizaje nguo hizo.
“Nguo hizi zinasambaza magonjwa ya kitropiki (Tropical Diseases) na kiwango kikubwa cha Watanzania wameathiriwa hasa na magonjwa ya ngozi,” alisema Manyilika.
Chanzo;Tanzania Daima 

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Kilimanjaro Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa