Home » » Watalii watapeliwa Kilimanjaro

Watalii watapeliwa Kilimanjaro

WATALII   wanane  raia wa Australia waliokuwa nchini kwa ajili ya kupanda mlima Kilimanjaro na kutembelea vivutio vya utalii katika visiwa vya Zanzibar, wamejikuta katika wakati mgumu baada ya kutapeliwa zaidi ya dola 7,000 za Kimarekani sawa na sh milioni 10.5 za Kitanzania na kampuni moja ya utalii mjini hapa.
Uchunguzi uliofanywa na Tanzania Daima umebaini kuwa kiasi hicho cha fedha kinajumuisha gharama za kupanda mlima Kilimanjaro, chakula na malazi kwa siku tatu na kutembelea vivutio vya utalii katika visiwa vya Zanzibar kwa siku tatu.
Tukio hilo limetokea Januari 9, mwaka huu baada ya wageni hao kupanda mlima Kilimanjaro kupitia lango la Machame, lakini baada ya kuteremka mlimani Januari 15, watalii hao walizuiliwa na maofisa wa Hifadhi ya Taifa ya Mlima Kilimanjaro (KINAPA) katika lango la Mweka wakidaiwa malipo ya siku tano.
Pamoja na watalii hao kujitetea kuwa walikuwa tayari wameshalipa gharama zote za kupanda mlima huo kwa siku saba, bado maofisa wa KINAPA waliendelea kuwashikilia hadi hapo walipofanya mawasiliano na wenzao Australia na kutumiwa fedha na hatimaye kulipa dola 4,800 sawa na sh 7,680,000 kutokana na kampuni hiyo kulipa malipo ya siku mbili tu.
Wakati hali ikiwa hivyo, Mkurugenzi wa Kampuni hiyo (jina limehifadiwa), kwa muda wa wiki mbili sasa amekuwa hapatikani ofisini kwake tangu kutokea kwa tukio hilo na simu zake zote za kijangani zimekuwa zikizimwa muda wote huku akimtumia mtu mmoja aliyejitambulisha kwa jina moja (tunalo) kumsemea.
Kutokana na tukio hilo, watalii hao walilazimika kufuta safari yao ya kutembelea vivutio vya utalii visiwani Zanzibar kutokana na mwenyeji wao kuingia mitini huku wapagazi wakishikilia vifaa vya kupandia mlima huo kutokana na kampuni hiyo kutowalipa mishahara yao.
Mbali na watalii hao, watalii wengine saba raia wa Sweden, nao wamejikuta wakionja joto ya jiwe baada ya kushilikiwa kwa zaidi ya saa kumi katika lango la Mweka baada ya kudaiwa malipo ya siku moja kutokana na kampuni iliyowapandisha mlima huo kulipa malipo ya siku sita badala ya saba.
Watalii hao walipanda mlima Kilimanjaro Januari 4  kupitia lango la Machame na kushuka Januari 10  kupitia kwa mfanyabiashara mmoja Filbert Laswai aliyenunua  vocha kutoka Kampuni ya Kili Boy’s na kupewa kibali namba 125219.
Akizungumza na Tanzania Daima mwishoni mwa wiki, Laswai alikiri kutokea kwa tukio hilo huku akijitetea kuwa tatizo hilo lilitokana na  mshirika wake kibiashara raia wa Kenya ambaye hakumtaja jina kuchelewesha malipo.
Mfanyabiashra huyo ambaye ni mtoto wa mfanyabiashara maarufu mjini hapa, Epmark Laswai, pia alikiri kudaiwa vifaa vya kupandia mlima na kampuni ya ukodishaji vifaa ya ASCEND Tanzania vyenye thamani ya sh 662,000.
Wapagazi waliotumika kubeba mizigo ya watalii hao vikiwamo vyakula, nao wameshikilia vifaa vya kampuni hiyo wakidai mishahara yao inayokadiriwa kufikia sh 2,755,000.
Hata hiyo meneja uhusiano wa Shirika la Hifadhi za Taifa (TANAPA), Pascal Shelutete, kwa wiki mzima amekuwa hatoi ufafanuzi juu ya matukio ya watalii  kutapeliwa na kampuni hizo licha ya mwandishi wa habari hizi kumtumia ujumbe mfupi wa maandishi mara kwa mara bila mafanikio.
Kwa upande wake Mkurugenzi wa kampuni ya ASCEND Tanzania inayojihusisha na ukodishaji wa vifaa vya mlimani, Fred Namwandu, amedai kupata hasara kubwa kutokana na vifaa vyake kushikiliwa na wapagazi kwa zaidi ya wiki tatu sasa huku pia kampuni hizo zikishindwa kumlipa fedha zake.
Chanzo;Tanzania Daima

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Kilimanjaro Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa