Home » » Gari la kigogo Bodi ya Kahawa lakamatwa Dar es Salaam

Gari la kigogo Bodi ya Kahawa lakamatwa Dar es Salaam

Gari binafsi la Mkurugenzi Mkuu wa Bodi ya Kahawa Tanzania (TCB), Injinia Adolf Kumburu lililoibwa na watu wasiojulikana mjini Moshi, Oktoba mwaka jana, limekamatwa jijini Dar es Salaam.
Habari za uhakika zilizothibitishwa na polisi, zilisema gari hilo aina ya Toyota Raum lilikamatwa na polisi, baada ya kulitafuta kwa miezi mitano mfululizo.
Gari hilo lililoibwa mjini Moshi Oktoba 4, 2013 lilikamatwa wiki iliyopita na limehifadhiwa katika Kituo cha Polisi cha Kawe cha jijini Dar es Salaam na watuhumiwa kadhaa nao wanashikiliwa.
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Kilimanjaro, Robert Boaz jana alithibitisha kukamatwa kwa gari hilo, kulikowezeshwa na kuwapo kwa taarifa za kiintelijensia za polisi na ushirikiano wa raia wema.
“Ni kweli Polisi tumefanikiwa kulikamata gari hilo likiwa limebandikwa nambari bandia na tayari mke wa Kumburu (hakumtaja kwa jina) ameshalitambua gari hilo pale Kawe,” alisema Boaz.
Katika wizi huo uliotokea kati ya saa 6:00 na saa 7:00 mchana nyumbani kwa mkurugenzi huyo eneo la Shanty Town mjini Moshi, vitu vingine vyenye thamani ya mamilioni ya shilingi pia viliibwa.
Kumburu aliwahi kukaririwa na gazeti hili mwaka jana akitaja vitu vingine kuwa ni runinga aina ya Samsung Flat Screen inchi 36, Deck aina ya Phillips, Micro-Wave, kompyuta mpakato aina ya Apple Mac Book, Samsung Min-Tablet na Digital kamera mbili.
Pia wezi hao waliiba simu mbalimbali za familia zipatazo nne moja ikiwa ni Blackberry na tatu aina ya Nokia na redio ndogo inayoshika masafa ya kimataifa, begi kubwa la nguo na jozi za viatu.
Chanzo;mwananchi
Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399.

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Kilimanjaro Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa