Home » » KIA yajizatiti kukabili dawa za kulevya

KIA yajizatiti kukabili dawa za kulevya

UONGOZI wa Kiwanja cha Ndege cha Kimataifa cha Kilimanjaro (KIA) umeahidi kuongeza jitihada za kupigana dhidi ya usafishaji wa dawa za kulevya kutokana na maboresho yaliyofanyika katika kitengo cha usalama cha uwanja huo.
Tamko hili limekuja siku chache baada ya Mtanzania, Mastura Makongoro, mwenye hati ya kusafiria namba AB26695 kukamatwa na dawa za kulevya zinazodhaniwa kuwa ni cocaine, zenye uzito wa kilogramu 4.8, akielekea Ghana.
Taarifa iliyotolewa jana na Mkurugenzi wa Fedha na Huduma za Kibiashara wa Kilimanjaro Airports Development Company (KADCO), Bakari Murusuri, ilieleza uwanja huo umejizatiti kupigana na usafarishaji wa dawa za kulevya kupitia uwanja huo.
Murusuri alisema maofisa usalama wa uwanja huo, Jumanne usiku wa manane walimkamata mwanamke huyo wakati akisubiri kupanda ndege ya Shirika la Ethiopia kuelekea mjini Addis Ababa.
Alisema wakati wa uchunguzi, mwanamke huyo alitubu kuwa aliambatana na mwenzake raia wa Nigeria, Mike Nwankwo (41), ambaye alimsindikiza mpaka uwanjani na alikuwa ni miongoni mwa mtandao wa wasafirishaji wa dawa hizo.
“Jeshi la Polisi na walinzi wa usalama hapa uwanjani waliunganisha nguvu ili kumsaka mtu huyo na baadaye alikutwa kwenye maegesho ya magari akisubiri kuhakikisha mwanamke huyo ameondoka nchini,” aliongeza.
Murusuri alisema tangu Machi mwaka jana mpaka sasa uwanja huo wa ndege umefanikiwa kukamata watu tisa wakihusishwa na usafirishaji wa dawa za kulevya na kuahidi kuwa uwanja huo umejizatiti kikamilifu kukabiliana na suala hilo.
Chanzo;Tanzania Daima
Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399.

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Kilimanjaro Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa