Lusekelo alisema siyo lazima Katiba Mpya ipatikane
mikononi mwa Rais Kikwete kwa kuwa hatua iliyofikiwa kwa sasa ni kubwa,
hivyo inaweza kuendelezwa na Rais atakayefuatia mwaka 2015.
Akizungumza jana katika ibada ya Pasaka, Lusekelo
alisema hali inayoendelea kwa sasa inajenga hofu na kuwachanganya
Watanzania kutokana na hofu ya Uchaguzi Mkuu ujao.
Alisema Bunge la Katiba kwa sasa limekuwa mfano wa
klabu ya pombe za kienyeji kutokana na vurugu alizodai kuchangiwa na
wajumbe wa CCM.
“Hakuna majadiliano ya kujenga hoja na badala yake
tunasikia matusi tu yanarushwa... uamuzi wa Profesa Ibrahim Lipumba
kutoka nje ulikuwa ni sahihi. Hata mimi iwapo ningekuwa mjumbe,
ningekuwa wa kwanza kutoka,” alisema Lusekelo na kuongeza:
“Kwa hiyo ni vyema mchakato ukasitishwa kwa hatua iliyofikia ili Taifa litulie na wananchi wajiandae kwa Uchaguzi Mkuu ujao.”
Iwapo mchakato huo hautasitishwa, alipendekeza
busara zitumike kuunda jopo la watu kutoka Usalama wa Taifa na wataalamu
wa masuala ya kiuchumi ili kujadili hoja tata ya muundo wa Serikali.
Alisema wachumi wanaweza kutafsiri hali ya
uendeshaji wa uchumi wa nchi endapo serikali tatu zitapitishwa huku watu
wa usalama wakitafsiri usalama wa nchi endapo muundo wa serikali mbili
utakufa.
“Watu wa usalama wanaifahamu nchi hata kwa miaka
30 ijayo, wanajua usalama wa taifa hili utakuwaje, kwa hivyo wakikaa na
wachumi wanaweza kuja na mapendekezo mapya tufanyeje,” alisema Lusekelo.
Lusekelo alisema: “Rais alikuwa na nia njema
kabisa baada ya kuruhusu mchakato huu uanze, lakini kabla ya kuunda Tume
inaonekana hakuwa amezungumza na chama chake juu ya mchakato wa Katiba,
kwani kama angekuwa amewashirikisha yote haya yasingejitokeza.
“Tume aliyoiteua ilikuwa na watu makini sana
kuanzia Mwenyekiti wake Jaji Joseph Warioba ambaye alikuwa Mwanasheria
Mkuu wa Serikali, Jaji Mkuu mstaafu Augustino Ramadhani na wenzake, ni
wasomi wa sheria kwa hivyo walikaa na kuchambua mpaka wakaona muundo wa
serikali tatu ndiyo unafaa.”
Alisema tatizo kubwa linalojitokeza ni pamoja na
wajumbe wa CCM kulazimisha muundo wa serikali mbili ikiwa ni tofauti na
uchambuzi uliofanywa na Tume hiyo.
Kakobe alia na Tanganyika
Kwa upande wake, Askofu Mkuu wa Kanisa la Full
Gospel Bible Fellowship, Zachary Kakobe ametangaza kuungana na wanaodai
Serikali ya Tanganyika na kuahidi kujenga ari na shauku ya kuhakikisha
inarejeshwa.
Akizungumza wakati wa ibada ya Pasaka iliyofanyika
kanisani hapo jana, Askofu Kakobe alisema anafanya hivyo si kwa
ushabiki ila ni kutokana na mipango ya Mungu, ambayo iliwezesha kuwapo
kwa Tanganyika huru. Huku akishangiliwa na waumini wa kanisa hilo,
Askofu Kakobe alisema wanaoidai Tanganyika katika Bunge la Katiba wapo
sahihi na yeye anaungana nao na kuwa wanaopinga wamekosa hofu ya Mungu.
“Serikali ilitumia mamilioni ya shilingi
kuadhimisha miaka 50 ya Uhuru, lakini wanashindwa kutamka uhuru wa nchi
gani!” alisema na kuongeza kuwa nchi imekosa utambulisho na hata Ziwa
Tanganyika linawasuta kwa kuwa katika uumbaji kuna mipaka ya asili,
ambayo inatambuliwa pia kitaalamu.
Kuzuia mabadiliko
Askofu wa Kanisa la Tanzania Assemblies of God
(TAG), mjini Moshi, Kilimanjaro, Glorious Shoo amewatahadharisha wajumbe
wa Bunge la Katiba kutotumia wingi wao bungeni kuzuia mabadiliko ya
Katiba.
Akizungumza katika ibada ya Jubilee ya miaka 75 ya
kanisa hilo, Askofu Shoo alisema umefika wakati ambao Watanzania
wanataka mabadiliko, hivyo wajumbe wa Bunge Maalumu wasitumie wingi wao
kuzuia mabadiliko.
“Tusilazimishe kwa wingi wetu kuzuia mabadiliko
kwa sababu ukweli tunaposema wingi wetu ni pale bungeni tu, lakini wingi
wetu sisi tulioko nje tunasikia kelele nyingi zinazolazimisha
mabadiliko naiomba Serikali izingatie hilo,” alisema Askofu Shoo.
“Watu wanaosoma nyakati, wanajua ukifika wakati wa
mabadiliko hakuna anayeweza kuzuia na ukijaribu kuyazuia mabadiliko
hayo yanakuja kukubadilisha wewe,” alisema Askofu Shoo.
Akizungumza katika ibada hiyo, Naibu Waziri wa
Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (Tamisemi), Aggrey Mwanri aliwaomba
viongozi wa madhehebu ya dini kufunga na kuliombea Bunge Maalumu la
Katiba ili liweze kuifanya kazi ya kuchambua Rasimu ya Katiba kwa hekima
itakayowapa Watanzania Katiba wanayoitaka.
Chanzo:Mwananchi
Chanzo:Mwananchi
0 comments:
Post a Comment