Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399.
MTOTO Samir anayekadiriwa kuwa na umri wa miaka minne hadi mitano,
mkazi wa Mtaa wa Langoni katika Manispaa ya Moshi, amekuwa akifungwa
kamba mguuni na bibi yake kwa lengo la kumzuia asiende kucheza mbali.
Tukio hilo limebainika hivi karibuni katika eneo hilo ambapo bibi
huyo ambaye hakufahamika jina alikutwa akiwa amemfunga kamba ya mguu
mjukuu wake huyo huku sehemu nyingine ikiwa imefungwa katika chuma
kizito.
Kwa mujibu wa majirani walisema bibi huyo amekuwa akimfunga mtoto
huyo mara kwa mara kwa zaidi ya nusu saa hasa nyakati ambazo bibi huyo
amekuwa akifanya shughuli zake za usafi wa ndani pamoja na kufua.
Wakizungumza kwa sharti la kutotajwa majina, majirani hao walisema
imekuwa ni kawaida kwa bibi huyo ambaye anaishi na wajukuu zake
kumfanyia kitendo hicho mtoto huyo huku akimzuia kucheza na wenzake wa
nyumba za jirani.
“Sisi hiyo hali mbona tumeizoea mara kwa mara Samir akienda kucheza
na wenzake huko mitaani, bibi yake akimkuta anamkamata na kisha
kumfunga kwenye hilo chuma lililoko hapo mlangoni kwa zaidi hata ya
nusu saa,” alisema mmoja wa majirani.
Akizungumza tukio hilo, bibi huyo ambaye anakadiriwa kuwa na miaka
zaidi ya 60 alikiri kumfunga mtoto huyo kwa madai amekuwa mtundu kupita
kiasi na kwamba ametumia mbinu hiyo ili kumdhibiti asitoroke nyumbani.
“Hapa nyumbani naishi na wajukuu zangu, wengine wako shuleni na
wengine wako kazini ambao ni wazazi wa huyu Samir, mmoja anafanya kazi
Arusha, mwingine yuko hapo mjini (Moshi) sasa sina mtu wa kunisaidia
kumwangalia huyu mtoto,” alisema bibi huyo.
Alisema analazimika kumfunga kamba mtoto Samir kutokana na kuwa na
tabia ya kwenda kuzurura katika nyumba za watu huku wakati mwingine
huenda kucheza mbali na nyumbani, jambo ambalo humpa shida kumpata kwa
urahisi.
Chanzo;Tanzania Daima
0 comments:
Post a Comment