Home » » RC GAMA:TUWEKE SIASA PEMBENI KUISAIDIA PANONE

RC GAMA:TUWEKE SIASA PEMBENI KUISAIDIA PANONE

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 
MKUU wa Mkoa (RC), wa Kilimanjaro, Leonidas Gama, amewataka wapenzi wa soka mkoani hapa kuweka siasa pembeni na badala yake waungane kuisaidia Klabu Bingwa ya Mkoa, Panone FC inayojiandaa na mashindano ya Ligi ya Mabingwa Mkoa (RCL), inayotarajiwa kuanza kutimua vumbi hivi karibuni.
Gama ambaye ni mlezi wa klabu mkoani hapa, alitoa rai hiyo juzi wakati akijibu kilio cha waandishi wa habari wa michezo Kilimanjaro, ambao wengi walimtaka mkuu huyo kuhakikisha ofisi yake inasimamia juhudi zote kuhakikisha klabu hiyo inapanda daraja.
Akizungumza katika tafrija fupi ya chakula pamoja na waandishi wa habari, Gama alisema mwaka huu ofisi yake imejipanga kuhakikisha Panone inafikia mafanikio yaliyofikiwa na Mbeya City na kuwataka wakurugenzi na wakuu wa wilaya zote sita, kuwa tayari kwa kazi hiyo.
“Natambua ni kiasi gani mlivyo na uchungu na maendeleo ya soka mkoani hapa, nitahakikisha timu hii inafanya vizuri, niwaombe viongozi wenzangu bila kujali itikadi zetu, tuungane kwa hali na mali tuibebe klabu hii,” alisema.
Gama ambaye amekuwa chachu ya kufufuka kwa hamasa ya michezo mkoani hapa, alisema mwaka huu wamejifunza kutokana na makosa ya mwaka jana wakati Machava wakiwa mabingwa, na kwamba safari hii kwa kushirikiana na Chama cha Soka Mkoa (KRFA), atajitahidi kufanikisha azma hiyo.
“Mwaka jana tuliteleza kwa Machava, ni ukweli usiopingika kwamba pamoja na tatizo la kiuongozi lililojitokeza katika klabu ile, siasa zilichangia pakubwa kwa timu yetu kushindwa kupanda Daraja la Kwanza na baadaye Ligi Kuu,” alisema Gama.
Wakizungumza katika hafla hiyo, waandishi Henry Lyimo, Dixon Busagaga na Yusuph Mazimu, walimtaka Gama kuishauri Panone kuangalia upya, kusuka uongozi wake na ikiwezekana kuunda kamati maalumu ambayo itafanya kazi bega kwa bega na uongozi wa Panone kuhakikisha inafanya vizuri.
Chanzo:Tanzania Daima

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Kilimanjaro Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa