Home » » WANACHAMA CHADEMA WAONYWA

WANACHAMA CHADEMA WAONYWA

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399. 
 
MWENYEKITI wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA), Mkoa wa Kilimanjaro na Mbunge wa Moshi Mjini, Philemon Ndesamburo, amewaonya baadhi ya Wanachama wa chama hicho wenye lengo la kukivuruga kwa misingi ya kiitikadi.
Ndesamburo, alitoa onyo hilo wakati akifunga mkutano mkuu wa CHADEMA Jimbo la Moshi Mjini uliyokwenda sanjari na uchaguzi wa kupata viongozi wa jimbo hilo pamoja na mabaraza, juzi.
Alisema, kutokana na umoja uliyopo ndani ya CHADEMA Moshi Mjini, baadhi ya watu kutoka nje ya chama wamekuwa wakijaribu kuwatumia wanachama wa chama hicho kutaka kuwagawa katika misingi ya kiitikadi.
“Tumejaribiwa sana na watu kutaka kutugawa kwa udini, kutugawa kwa ukabila, wanashangaa Jafary ni Mpare lakini ndiye Meya wetu, wengine wanasema eti Meya Muislamu, sisi hatuchagui watu kwa sura zao wala wanakotoka,” alisema Ndesamburo.
Aliutaka uongozi mpya uliochaguliwa juzi, kuanza kazi mara moja ya kukiimarisha chama kuanzia ngazi ya mashina na kwamba, hadi kufikia uchaguzi mkuu mwakani CHADEMA iweze kukamata dola.
“Ndugu zangu mmechaguliwa, sio kazi ya mchezo, msifurahie nafasi mlizopata mkadhani ni lele mama, mmechaguliwa mkafanye kazi, sitegemei kusikia mtu anasema sina nafasi, imani yangu kubwa kwa sasa tumepata timu ya kuchapa kazi, tunataka Jimbo la Moshi liendelee kubaki CHADEMA,” alisema Ndesamburo.
Naye Katibu wa CHADEMA Kanda ya Kaskazini, Aman Golugwa, aliwataka wazee wa Chama kwa hekima na busara zao, kuwashughulikia wanachama watakaobainika kutaka kusababisha vurugu ndani ya chama.
“Uchaguzi umekuwa na heka heka nyingi, nafahamu kwa sasa tunaelekea katika chaguzi za serikali za mitaa na uchaguzi mkuu, kwa wale wanaotaka nafasi ya uongozi msituletee fujo, unataka nafasi ya uongozi ingia kwenye mfumo wa chama, halafu tukupe nafasi ufahamike watu wakujue,” alisema Golugwa.
Katika uchaguzi huo, Mstahiki Meya wa Manispaa ya Moshi, Jafary Michael, alifanikiwa kutetea nafasi yake ya Uenyekiti wa Jimbo la Moshi Mjini baada ya kukosa mpinzani katika nafasi hiyo.
Katibu wa CHADEMA Jimbo la Moshi Mjini, alichaguliwa Stephen Buberwa, Katibu Mwenezi Steven Ngasa huku mjumbe wa mkutano mkuu taifa akiibuka Peter Msafiri.
Kwa upande wa wajumbe wanne wa Kamati ya Utendaji, walichaguliwa Shaffi Ally, Cosmas Tesha, Paulo Minja na Aisha Rashid huku Baraza la Vijana (Bavicha), wakichaguliwa Dominick Tarimo nafasi ya Uenyekiti, Deogratius Kiwelu alishinda Ukatibu na Steven Urio Mhamasishaji Vijana.
Baraza la Wanawake walichaguliwa Mary Olomi (Mwenyekiti), Ovena Kowero (Katibu), Anna Mushi (Uenezi), na Nice Mushi (Mhazini).
Kwa upande wa Baraza la Wazee, walichaguliwa Ally Mwamba (Mwenyekiti), Augustino Makelele (Mwenyekiti msaidizi), Ahmad Ndaile (Katibu), na Mlavi Mrindoko (Mhazini)
Uchaguzi huo ni muendelezo wa chaguzi zinazoendelea nchi nzima, baada ya kumaliza chaguzi za misingi, matawi na kata, ambako sasa hatua inayoendelea ni ya ngazi ya majimbo/wilaya kuelekea Mikoa na Kanda, kabla ya uchaguzi wa viongozi wa kitaifa unaotarajiwa kufanyika baadaye mwaka huu.
Chanzo:Tanzania Daima 

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Kilimanjaro Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa