Home » » KNCU WAMLAUMU MRAJISI WA VYAMA

KNCU WAMLAUMU MRAJISI WA VYAMA

Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399.

Chama Kikuu cha Wakulima wa Kahawa Mkoa wa Kilimanjaro (KNCU), kimemjia juu mrajisi wa vyama hivyo nchini kwa kile ilichodai kukwamisha ustawi na maendeleo yake.
Kauli hiyo ilitolewa mwishoni mwa wiki na mwenyekiti wa KNCU, Maynard Swai wakati akisoma hotuba yake katika mkutano mkuu maalumu ulioitishwa kwa shinikizo la mrajisi huyo, Dk Audax Rutabanzibwa.
Licha ya kupokea lawama hizo, Dk Rutabanzibwa aliyekuwa mwenyekiti katika mkutano huo hakuweza kujibu malalamiko yaliyoelekezwa kwake na mwenyekiti huyo.
Mwenyekiti huyo aliwaachia wajumbe wa mkutano huo kufanya uamuzi kwa njia ya kura kama bodi ya uongozi iendelee au ing’oke ambapo kura 83 zilikataa na 68 zikitaka ing’oke.
Swai alisema ofisi ya mrajisi huyo imekuwa kikwazo cha maendeleo kwa KNCU .
“Mfano, shamba la Garagagua lilitakiwa kuuzwa Mei 2014, wajumbe mlisharidhia lakini kutokana na ukiritimba wa ofisi ya mrajisi imekwama,” alisema Swai. Swai aliitaja mipango mingine kuwa ni ujenzi wa hosteli ya kisasa na hoteli kwenye eneo la makao makuu ya KNCU.
“Sina nia ya kuifundisha au kuikumbusha ofisi ya Mrajisi wajibu wake kiutendaji lakini ina wajibu wa kushauri na kusimamia ushirika ili uendelee kushamiri nchini kwa manufaa ya wanachama,”alisema.
Lakini Swai alisema hata tume mbalimbali za uchunguzi zilizotumwa KNCU katika kipindi kifupi cha miaka miwili na Mrajisi, hazijawahi kutoa mrejesho wa matokeo ya uchunguzi huo.
“Kifungu 57(1) cha sheria namba 6 ya Ushirika ya mwaka 2013 imeweka bayana kuwa ikiwa kuna uchunguzi au ukaguzi umefanywa dhidi ya chama cha Ushirika, Mrajisi atapaswa kutoa matokeo ya uchunguzi huo,”alisema Swai.
KNCU kimeshangazwa pia na hatua ya Mrajisi kutoamini ukaguzi uliofanywa na COASCO ambacho ni chombo cha Serikali kuhusu kiasi cha hasara ambayo KNCU ilipata wakati wa mdororo wa uchumi duniani mwaka 2008.
Katika hesabu hizo, KNCU ilionyesha kupata hasara ya zaidi ya Sh765 milioni wakati uhakiki uliofanywa na hazina ulionyesha KNCU kilipata hasara ya Sh250 milioni.
“Mrajisi aliagiza kufuatiliwa kwa tofauti hii huku akionesha kutokuwa na imani na hesabu zilizokaguliwa na COASCO jambo ambalo linashangaza kama Serikali haiwezi kuamini kazi iliyofanywa na chombo chake,” alisisitiza Swai.
Chanzo;Mwananchi

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Kilimanjaro Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa