Home » , » Kilimanjaro Marathon 2015 kufanyika Machi 1,mjini Moshi

Kilimanjaro Marathon 2015 kufanyika Machi 1,mjini Moshi


Mbio za 13 za Kilimanjaro Marathon ambazo zimepangwa kufanyika Machi 1, 2015 mjini Moshi mkoani Kilimanjaro zimepata msisimko mpya baada ya wanariadha nyota wa Tanzania kuthibitisha kushiriki.

Mkurugenzi wa Mbio hizo John Bayo jana katika taarifa yake kwa vyombo vya habari aliwataja baadhi ya wanariadha nyota kutoka Tanzania kuwa ni Andrew Sambu, Daudi Joseph, Mashaka Masumbuko, watachuana na wanariadha wengine kutoka nchini na kutoka nje ya nchi katika mbio za Kilimanjaro Premium Lager Marathon kwa wanaume za kilometa 42.195.

Kwenye upande wa marathon wanawake Fabiolla William, Sarah Maja and Banuelia  Katesigwa ni miongoni mwa nyota wa Tanzania watakaochuana na wenzao kutoka ndani na nje ya nchi katika kuwania tuzo mbalimbali kwenye Mbio za Kilimanjaro Premium Lager Marathon kwa wanawake za Kilometa 42.195.

Aidha, wanariadha Fabian Fabian Joseph, Alphonce Felix, Dickson Marwa wamethibitisha kushiriki Tigo Kili Half Marathon wanaume wakati Mary Naali, Natalia Elisante, Catherine Lange na Jacqueline Sakilu ni miongoni mwa majina maarufu katika riadha yaliyothibitisha kushiriki kupitia kundi la wanawake litakalochuana katika Mbio za Tigo Kili Half Marathon.

Katika mbio za nusu marathon ambazo Tanzania ina historia ya kufanya vizuri, Fabian Joseph ana rekodi ya ushinda Kilimajaro Marathon mwaka 2010 ambapo alimaliza mbio katika muda wa 1:3;59 na vilevile ana rekodi ya kushinda Edmonton Marathon mwaka 2005 kwa muda wa 1:01:08.

Akiwa ametengeneza rekodi nyingi, Mary Naali ni kati ya wanariadha bora nchini katika mbio za kilomita 21 maarufu kama Half Marathon. Alishinda Vienna Marathon mwaka 2010 ambapo alimaliza katika muda wa 1:12:16 na baada ya hapo akavunja rekodi kwenye mbio za kilomita 25 za Arusha VIP Race mwaka 2011 ambapo alishinda kwa 1 1:20:52 na kuvunja rekodi ya 1:22:18 iliyokuwa imewekwa na Josephine Deemay mwaka 2006. Mei mwaka 2013 pia alishinda mbio ya Bucharest International Marathonihuko Romania akimaliza katika muda wa 1:16:32.

Naali atachuana vikali na Jacqueline Sakilu ambaye ni bingwa mtetezi kutokana na ushindi wake kwenye 2014 Kilimanjaro Marathon ambapo alimaliza mbio akiwa na 1:12:43 ambayo bado ni rekodi yake katika mbio hizo.

Bayo alisema kwamba Sakilu ni kati ya wanariadha ambao wana mvuto sana kutokana na umahiri na kujituma na anaweza kufanya makubwa kwa mara nyingine tena.

 “Tuna furaha kuwa na kikosi madhubuti kwa wanaume na wanawake,” alisema John Bayo ambaye pia ni kocha maarufu wa riadha. “Uwepo wa wanariadha hawa wazoefu naamini utaifanya mbio hii iwe ya kuvutia.”

John Addison, Mkurugenzi mku wa kampuni ya Wild Frontiers, inayoandaa Mbio za Kilimanjaro Marathon alisema kuwa takribani watu zaidi ya 6000 kutoka mataifa 40 ya mabara sita wanatarajia kushiriki katika maadhimisho ya kumi na tatu ya Mbio za Kilimanjaro Marathon.

Addison alisema kwamba mbio za mwaka huu zinatarajiwa kuwa na vivutio pamoja na motisha mbalimbali kwa washiriki ambapo medali na tisheti zitatolewa kwa washiriki 500 wa kwanza kumaliza mbio za kilomita 42, washiriki 2,200 na washiriki 80 wa mbio za walemavu za GAPCO watapata tisheti na medali.

Mbio hizo zinaratibiwa na Executive Solutions kwa kushirikiana na Riadha Tanzania, Chama cha Riadha Kilimanjaro, Kilimanjaro Marathon Club chini ya udhamini wa Kilimanjaro Premium Lager, Tigo, GAPCO, Simba Cement, na KK Security, Keys Hotel, TPC Sugar,  CMC Automobiles Ltd, RwandAir, FNB Tanzania, Kibo Palace Hotel, UNFPA na Kilimanjaro Water.
Ikiwa unatukio lolote au jambo lolote tuma kupitia Barua pepe yetu blogzamikoa@live.com au Whatsapp namba +255765056399.

0 comments:

 
Supported by Tone Multimedia Company Limited
Copyright © 2012. Kilimanjaro Yetu - All Rights Reserved
Designed by Fredy Tony Njeje
Proudly powered by Blogs za Mikoa